Na Saida Issa,Dodoma
WAZIRI Mkuu, Mhe.Kassim Majaliwa amezitaka Wizara, Idara na Taasisi za Serikali kufanya kazi kwa karibu na Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali katika uendeshaji wa mashauri ya madai na usuluhishi yanayohusu Serikali kwani ndiyo yenye mamlaka ya kisheria ya kusimamia mashauri yanayohusu Serikali na Taasisi zake ndani na nje ya Nchi kufanya hivyo kutasaidia kupunguza gharama kwa serikali.
Hayo aliyasema Jijini Dodoma katika Maadhimisho ya Miaka Mitano ya Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali na Uzinduzi wa Mafunzo kwa Mawakili wa Serikali ambapo aliwataka watendaji wa idara na taasisi zote za Serikali kutekeleze majukumu yao kwa kuzingatia sheria hususan katika huduma wanazozitoa na miradi wanayoisimamia ili kuiepusha Serikali kuingia katika migogoro ambayo inaweza kuepukika.
"Nawaagiza Watendaji wote wa Serikali zingatieni sheria, taratibu na kanuni tulizojiwekea kwenye utekelezaji wa majukumu yetu ikiwemo usimamizi wa mikataba na makubaliano mbalimbali tunayoingia ili kuepusha migogoro isiyo ya lazima inayoweza kutokea ndani ya Serikali na kusababisha kufunguliwa kwa mashauri ya madai na usuluhishi,"alisema Majaliwa.
Waziri Mkuu alisema kuwa Mawakili wa Serikali wamepewa dhamana kubwa ya kuitetea Serikali katika uendeshaji wa mashauri ya madai na usuluhishi, hivyo waongeze bidii na juhudi katika utendaji kazi na wafanye kazi kwa uzalendo, weledi na uadilifu.
“Serikali kwa upande wake itaendelea kuitengea bajeti ya kutosha Ofisi hii kwa kadri rasilimali zitakavyoruhusu. Vilevile, itaendelea kuipatia rasilimali watu ya kutosha sambamba na kuwezesha upatikanaji wa mafunzo kwenye maeneo ya kimkakati kama vile mafuta na gesi, uwekezaji, sheria za anga na madini,"alisema Waziri Mkuu.
Waziri Mkuu alisema ili kuhakikisha kuwa Serikali inaendelea kuimarisha diplomasia ya uchumi na kuendelea kujenga mazingira shindani ya kuvutia wawekezaji, Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali kwa kushirikiana na Wizara, Idara na taasisi za Serikali itatue migogoro kwa njia ya majadiliano na maridhiano.
Kwa upande wake, Waziri wa Katiba na Sheria, Dkt. Damas Ndumbaro alisema katika kipindi cha miaka mitano tangu kuanzishwa kwa ofisi hiyo ambayo inafanya kazi kwa weledi imeweza kuisaidia Serikali kuokoa zaidi ya shilingi trilioni saba kutokana na kutatua baadhi ya mogogoro kwa njia ya usuluhishi.
Huku Wakili Mkuu wa Serikali, Dkt. Boniphace Luhende alisema baada ya uzinduzi huo wanatarajia kuendesha mafunzo ya siku tatu kwa Mawakili wa Serikali zaidi ya 600 ili kuwaongezea ufanisi katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku.
0 comments:
Post a Comment