METDO Tanzania

METDO Tanzania

Monday, August 1, 2022

DC MWEMA AMEWATAKA MAKARANI, WASIMAMIZI WA MAUDHUI NA TEHAMA KUZINGATIA MAFUNZO YANAYOTOLEWA ILI KURAHISISHA ZOEZI LA SENSA



Na Maganga Gwensaga – Dodoma

Mwenyekiti wa kamati ya Sensa ya Wilaya ya Kongwa na Mkuu wa Wilaya hiyo Mhe. Remidius Mwema amewataka makarani, wasimamizi wa maudhui na Tehama Kila mmoja kutambua  thamani ya uwepo wake katika mafunzo hayo, ajifunze kwa makini ili kufanya kazi hiyo kwa ufanisi mkubwa.

Mwenyekiti huyo alisema hayo Julai 31, 2022  wakati wa ufunguzi wa mafunzo ya makarani, wasimamizi wa Tehama na maudhui ambao watashiriki katika zoezi la sensa ya watu na makazi litakalofanyika nchini tarehe 23 Agosti mwaka huu.

“ Ndugu zangu naomba niwaeleze, wewe uliyeko hapa utambue thamani kubwa uliyopewa na Serikali ya kushiriki zoezi hili kubwa la Kitaifa ambalo linaenda kufanyika nchini kwetu na hauko hapa kwa bahati mbaya.” Alisema Mwema

Alisema zoezi la Sensa ni muhimu sana kwani ni maendeleo, ni elimu, ni barabara,  ni afya , ni umeme hivyo kuzingatia kwao mafunzo kutasaidia ukusanywaji wa taarifa sahihi za watu na makazi hivyo watairahisishia Serikali katika masuala ya kupanga mipango yake ya kimaendeleo ambayo imekusudia kuwapelekea wananchi wake.

“ Serikali inawategemea sana, usipozingatia mafunzo ukafanya mzaha katika jambo hili na mwisho wa siku ukafanya ndivyo sivyo, zoezi letu likaharibika wewe ndio utakuwa  sababu kumbuka sio Kongwa tu, wala Dodoma bali utakua umeharibu taswira nzima ya zoezi hili Kitaifa na nisingependa yatokee hayo.” Aliongeza.

Aidha  aliwataka washiriki hao kuzingatia muda uliowekwa wa kuanza mafunzo ili muda uliotolewa na ofisi ya Taifa ya Takwimu uende sambamba na muda wa mafunzo ili yaweze kukamilika kwa wakati, uku akisisitiza kufanya kazi kwa weledi, kuwa na nidhamu pamoja na kuheshimiana.

“ Suala la nidhamu ni muhimu sana najua wengine mnatofautiana umri, vyeo nk hivyo ni vyema kuheshimiana, kuzingatia muda wa kuja, kuheshimiana wenyewe kwa wenyewe, kutii walimu wenu, kusikiliza kwa umakini na kujiepusha na vitendo vyote ambavyo viko kinyume na maadili.” Alisema

Kwa upande wao washiriki wa mafunzo hayo wamemuhakikishia Mwenyekiti huyo kuzingatia mafunzo yote watakayopewa na wakufunzi hao na wako tayari kushiriki na kufanikisha zoezi hilo.

Mafunzo ya makarani, wasimamizi wa maudhui na Tehama yalianza Julai 31 Agosti na yanatarajia kumalizika tarehe 18 Agosti nchi nzima ambapo kwa Wilaya ya Kongwa yamegawanywa katika vituo vinne(4) ambavyo ni Kongwa, Kibaigwa, Mlali na Mkoka ambapo yatatolewa kwa makarani 1197, Wasimamizi wa Tehama 22 na Wasimamizi wa Maudhui 24.

Ikumbukwe wilaya ya Kongwa ndio wilaya pekee ambayo itakuwa na matukio makubwa mawili siku hiyo, mosi uwepo wa zoezi la Sensa ya watu na Makazi pamoja na pili ni Mbio za Mwenge wa uhuru.

Share:

0 comments:

Post a Comment

Copyright © WAZO HURU | Powered by Blogger Design by ronangelo | Blogger Theme by NewBloggerThemes.com