METDO Tanzania

METDO Tanzania

Monday, March 8, 2021

Mbinga Girls:Sekondari ya wananchi inayofaulisha kwa asilimia 100



SHULE ya sekondari ya Mbinga Girls ambayo inamilikiwa na wananchi wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma imeendelea kupata mafanikio makubwa kitaaluma tangu kuanzishwa kwake mwaka 2014.

Mkuu wa shule hiyo Efigenia Nzota amesema shule hiyo yenye kidato cha kwanza hadi cha nne ilianzishwa kwa ajili ya wanafunzi wa kike ambapo ilianza kutoa wahitimu wa kidato cha nne mwaka 2017 kwa kufaulisha kwa asilimia 95 ambapo kati ya wahitimu 68 walifanya mtihani waliopata sifuri walikuwa watatu.

Nzota amesema mwaka 2018 jumla ya wanafunzi waliofanya mtihani wa kidato cha nne walikuwa 77  ambapo shule hiyo iliweza kufaulisha kwa asilimia 98 na kwamba ni mwanafunzi mmoja tu ndiyo alipata daraja sifuri.

“Mwaka 2019 tulikuwa na watahiniwa 108 ufaulu wetu ulikuwa kwa asilimia 100,matokeo haya ndiyo yaliyotuwezesha kupata tuzo baada ya kuingia katika shule kumi bora kitaifa katika kundi la shule za wananchi kwa kushika nafasi ya sita kati ya kumi’’,alisema.

Kwa mujibu wa Mkuu huyo wa shule,Mbinga Girls imeendelea kupata mafanikio makubwa kitaaluma ambapo mwaka 2020,shule hiyo ilifaulisha kwa asilimia 100 kutokana na watahiniwa 93 kufanya mtihani na kufaulu wote.

Ameitaja siri kubwa inayofanya shule hiyo kuendelea kufanya vizuri kitaalamu ni kila mwalimu kutekeleza majukumu yake bila kusukumwa ambapo amesema kuna wakati walimu wanafundisha hadi usiku na siku za Jumamosi na Jumapili.

Hata hivyo amesema matokeo hayo mazuri ya mitihani yanatoa picha nzuri kwamba shule hiyo  inakwenda vizuri kitaalum kwa sababu imefanikiwa kuondoa sifuri na kiwango cha ufaulu kinaendelea kupanda mwaka hadi mwaka.

“Matarajio yetu kama walimu tunatamani ifike mahali katika shule hii division four isiwepo kabisa,walau tuishie three,ili kufikia malengo yetu tunajenga mshikamano mkubwa baina ya walimu na tunasisitiza maadili kwa wanafunzi wetu ili kuwaleta kwenye ulimwengu wa kitaaluma’’,alisisitiza Nzota.

Ameutaja msingi mkubwa katika shule hiyo ni kujenga nidhamu kwa wanafunzi ambapo tangu shule hiyo imeanzishwa mwaka 2014 hadi 2021 jumla ya wanafunzi saba tu wameondolewa kwa ujauzito.

Shule ya sekondari Mbinga Girls ina walimu 19 na wanafunzi 453.

Share:

0 comments:

Post a Comment

Copyright © WAZO HURU | Powered by Blogger Design by ronangelo | Blogger Theme by NewBloggerThemes.com