Katibu Mkuu
Wizara ya Kilimo Bwana Gerald Kusaya leo tarehe 13 Agosti, 2020 ametembelea mkoa
wa Tabora kwa ajili ya kukagua na kujionea shughuli za maendeleo ya Sekta ya
Kilimo hususan tasnia ndogo ya zao la tumbaku na kumwambia Mkuu wa mkoa wa
Tabora Dkt. Philemon Sengati kuwa mkoa wake umepata upendeleo wa kupata zaidi
ya milioni 500 kwa ajili ya ujenzi wa miradi miwili.
Katibu Mkuu
Kilimo Bwana Kusaya amesema fedha hizo zitakwenda katika Halmashauri ya wilaya
ya Nzega Mjini na Nzega vijijini ambapo maeneo yatakayonufaika na pamoja na
kijiji cha Idudumo (Nzega Mjini) na kijiji cha Busondo (Nzega Vijijini).
Awali
katika taarifa yake ya maendeleo ya Sekta ya Kilimo; Mkuu wa mkoa wa Tabora
Dkt. Philemon Sengati amemwambia Katibu Mkuu Kusaya kuwa uzalishaji wa mazao ya
chakula na biashara umekuwa mzuri licha ya kukabiliwa mabadiliko ya tabia nchi
na kuiomba Wizara isaidie katika utaalam na mbegu bora na zenye kutoa matokeo
mazuri kwenye maeneo yenye ukame.
Kwa upande
wake Katibu Mkuu Kilimo Bwana Kusaya amemwambia mwenyeji wake kuwa Wizara
inafanya kazi karibu na Watendaji wengi wa mkoa wa Tabora ambapo, jana tarehe
12 Agosti, 2020 alitembelea Halmashauri ya Wilaya ya Nzega mjini na vijijini
kwa ajili ya utekelezaji wa miradi miwili mikubwa.
Katibu Mkuu
Kusaya aliutaja mradi wa kwanza ni ukarabati wa miundombinu ya skimu ya
uwagiliaji katika kijiji cha Idudumo Halmashauri ya wilaya ya Nzega mjini
ambapo Katibu Mkuu Bwana Kusaya alisema Wizara imetenga kiasi cha shilingi
milioni 100 (100,000,000) ambapo zitatumiaka kuanza ukarabati na ujenzi wa
mifereji ya Bwawa.
Mradi
mwengine ni ujenzi wa ghala ya kuhifadhia mazao ya kilimo; Ghala hilo lina
uwezo wa kuhifadhi tani 2,000. Katibu Mkuu Kusaya amesema Halmashauri ya Nzega
vijijini imepata fursa hiyo baada ya Mhe. Rais wa Awamu ya Tano, Dkt. John
Pombe Joseph Magufuli kutoa kiasi cha shilingi bilioni 80 kupitia Mradi wa
Kudhibiti Changamoto ya Sumukuvu (TANPAC).
Katibu Mkuu
Kusaya ameongeza kuwa fursa ya kujengewa maghala hayo imetoka kwenye Mradi wa
Kudhibiti Sumukuvu (TANPAC) ambapo jumla ya Halmashauri 12 za Tanzania Bara na
mbili (2) za Zanzibar zimenufaika kwa ujenzi huo wa maghala.
Katibu Mkuu
Bwana Gerald Kusaya amemwambia Mkuu wa mkoa wa Tabora, Dkt. Philemon Sengati
kuwa jana jioni alipitia ili kujionea eneo hilo katika kijiji cha Idudumo na
kijiji cha Busondo na kukagua maeneo hayo yote. Katika Kijiji cha Busondo jumla
ya Wanakijiji 22 wakiongozwa na Mwenyekiti wa Serikali ya kijiji Bwana Mustafa
Kasalu Maganga pamoja na Katibu Tawala wa kijiji hicho Bwana Laurent Mtunga
Iholong’wa waliridhia na kutoa hekari 5 kwa ajili ya ujenzi huo ambao unataraji
kuanza mwezi Disemba, 2020.
Akiongea
kwa niaba ya Wanakijiji wenzake Bibi Easter Msafiri amemshukuru Mhe. Rais
Magufuli kwa kuleta Mradi huo kwa wanakijiji wenzake.
“Napenda
kuishukuru Serikali ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Dkt. John Pombe Joseph
Magufuli kwa kuona umuhim wa kutuletea Mradi mkubwa kama huu; Hatukuwa na Mradi
kama huu hapo kabla”. Amekaririwa Bi. Easter Msafiri, mkazi wa kijiji cha
Busondo.
0 comments:
Post a Comment