METDO Tanzania

METDO Tanzania

Tuesday, May 19, 2020

DKT MABULA: BODABODA TUFANYE KAZI, TUJALI AFYA ZETU



Waendesha pikipiki maarufu kama bodaboda wametakiwa kutekeleza kwa vitendo kauli ya Rais Mhe Dkt  John Magufuli ya kufanya kazi wakati huo huo wakichukua tahadhari ya maambukizi ya ugonjwa wa Covid-19 unaoenezwa na  kirusi cha  Corona.

Ushauri huo umetolewa na Mbunge wa Jimbo la Ilemela Mhe Dkt Angeline Mabula katika viwanja vya shule ya msingi Buswelu wakati akizungumza na waendesha pikipiki wa wilaya ya Ilemela juu ya kuchukua tahadhari za maambukizi ya ugonjwa huo na kukabidhi vifaa vya kujikinga ikiwemo barakoa 1500, vitakasa mikono katoni 6 na sabuni za kunawia mikono ili viweze kugawanywa katika vituo vyote vya waendesha pikipiki kwa lengo la kujikinga na maambukizi mapya ya ugonjwa wa Covid-19

‘.. Suala la magonjwa sio jipya, tulikuwa na ukimwi, tuna malaria, kuna shinikizo la damu, Sasa hili la Corona lisitufanye tukashikwa na hofu mpaka tukafa kwa hofu badala ya ugonjwa wenyewe ..’ Alisema 

Aidha Mhe Dkt Angeline Mabula akatumia fursa hiyo kumpongeza Rais Mhe Dkt John Magufuli kwa kutofunga mipaka ya nchi na kuruhusu wananchi wake kuendelea na shughuli za kila siku huku wakichukua tahadhari dhidi ya ugonjwa huo sambamba na kuwataka waendesha pikipiki hao kujiunga na bima ya afya iliyoboreshwa ya gharama nafuu ICHF ambayo gharama zake ni shilingi elfu 30,000 kwa mwaka ikiwezesha kuhudumiwa bure katika zahanati na vituo vya afya kwa watu sita akiwemo baba, mama na watoto wanne 

Akimkaribisha mbunge huyo, Mwakilishi wa mkuu wa wilaya ya Ilemela ambae pia ndie afisa tarafa wa wilaya hiyo Bwana Godfrey Mzava amempongeza mbunge Mhe Dkt Mabula kwa kazi kubwa anazozifanya katika kuwaletea wananchi maendeleo na hasa uungaji mkono kwa serikali katika vita dhidi ya ugonjwa wa Covid-19 tangu kuanza kwake ambapo amekuwa akigawa vifaa vya kujikinga kwa makundi mbalimbali wakiwemo madereva, makondakta, polisi, viongozi wa dini, masoko, vyama vya siasa, na leo amegawa kwa waendesha pikipiki maarufu kama bodaboda.

Nae Diwani wa kata ya Buswelu ambae pia ni mwenyekiti wa kamati ya huduma ya manispaa ya Ilemela Mhe Sarah Ng’wani amemshukuru Mhe Dkt Angeline Mabula kwa juhudi zake katika kuhakikisha anatekeleza shughuli za maendeleo na kuwasisitiza waendesha pikipiki hao kutunza na kuvitumia vizuri vifaa vilivyotolewa.
 
Akihitimisha mwenyekiti wa waendesha pikipiki wilaya ya Ilemela Ndugu Makoye John Barinago mbali na kushukuru na kumpongeza mbunge huyo kwa msaada wake alioutoa akamuomba pia kuhakikisha anawasaidia bodaboda hao kupata eneo rasmi la kufanyia shughuli zao pamoja na kusaidia upatikanaji wa bima ya afya maombi ambayo yote yalipatiwa majawabu na mbunge huyo papo kwa hapo.

Kupitia zoezi hilo kwa niaba ya mganga mkuu wa wilaya ya Ilemela Bi Rose Nyemere alipata fursa ya kuelimisha jamii juu ya maambukizi ya ugonjwa wa Covid-19 na namna ya kujikinga.
Share:

0 comments:

Post a Comment

Copyright © WAZO HURU | Powered by Blogger Design by ronangelo | Blogger Theme by NewBloggerThemes.com