METDO Tanzania

METDO Tanzania

Friday, April 24, 2020

WIZARA YA KILIMO KUSHIRIKIANA NA SUA KUZALISHA MBEGU BORA ZA MAZAO


Katibu Mkuu Wizara ya Kilimo Bw.Gerald Kusaya akiongea wakati akikagua shamba darasa la zao la chai alipotembelea Chuo Kikuu cha Sokoine leo mjini Morogoro.Kulia kwake ni Dkt.Kudra Abdul Mkuu wa Idara ya Mimea Vipande na Kilimo cha Bustani.
Katibu Mkuu Wizara ya Kilimo Bw.Gerald Kusaya (katikati) akiongozana na Makamu Mkuu wa Chuo cha Sokoine Prof.Raphael Chibunda (kulia) kukagua miradi ya chuo hicho leo mjini Morogoro
Wakurugenzi wa Idara toka wizara ya Kilimo wakiwa kwenye kikao na Menejimeti ya Chuo Kikuu cha Sokoine na kujadili ushirikiano wa kuongeza tija na uzalishaji mazao nchini.
Katibu Mkuu Wizara ya Kilimo Bw.Gerald Kusaya akiwa ameshika mche wa nanasi wakati alipokagua shamba darasa la kufundishia wanafunzi chuo Kikuu cha Sokoine leo mjini Morogoro.Kushoto ni Bw.Ramadhani Omari Mhadhiri wa mafunzo ya bustani na wa kwanza kulia ni Makamu Mkuu wa Chuo cha SUA Prof.Raphel Chibunda.

 ya Kilimo imekubaliana na Chuo Kikuu cha Kilimo Sokoine kuanza kuzalisha mbegu bora za mazao ya kilimo ili kujitosheleza na mahitaji ya wakulima nchini.

Makubaliano hayo yamebainishwa leo (24.04.2020) na Katibu Mkuu Wizara ya Kilimo Gerald Kusaya alipokutana kwa mazungumzo na Menejimenti ya Chuo hicho mjini Morogoro na kueleza kuwa nchi bado haijajitosheleza na mbegu bora.

“Tunahitaji ushirikiano wa kuzalisha mbegu bora za mazao ya kilimo kwa wingi ndani ya nchi ili kukidhi mahitaji ya wakulima ” alisisitiza Katibu Mkuu

 Wizara ya Kilimo inapenda chuo Kikuu cha Sokoine  kianzishe vitalu vya uzalishaji mbegu bora za mazao ya mboga mboga na matunda ili kupunguza utegemezi toka nje ya nchi.

“Ifike hatua nchi yetu kuwa na uhakika wa mbegu bora na hai.Hii itaongeza ajira kwa vijana na wakulima kupata manufaa” alisema Katibu Mkuu Kusaya

Kusaya alitaja maeneo mengine ya ushirikiano na Chuo Kikuu cha Sokoine kuwa ni  kuanzisha maabara bora ya kilimo ili kusaidia mapinduzi katika utafiti,uanzishwaji wa mashamba darasa kwa wahitimu wa masomo ya kilimo na kujenga maabara ya kisasa ya kupima ubora wa mazao yakiwemo mboga mboga na matunda kabla ya kusafirisha nje ya nchi ili kuongeza thamani ya bidhaa za kilimo.

Pia uhamasishaji matumizi ya teknolojia ya bora ya uzalishaji kwa kutumia zana za kisasa na utoaji huduma za ugani na mafunzo ya muda mfupi kwa wataalam wa wizara  na wakulima kwa kutumia vyombo vya habari na TEHAMA ,Ili kuwa na kilimo chenye tija na manufaa kwa mkulima ,Katibu Mkuu Kusaya amekiomba chuo cha Sokoine kusaidia jitihada za wizara kudhibiti visumbufu vya mimea na mazao kama viwavijeshi,ndege waharibifu wa kwerea kwerea,nzige wa jangwani,panya na magugu yanayoathiri mazao ya wakulima.

“Tunahitaji sifa nzuri ya ubora wa mafunzo na wataalam wa  chuo kikuu cha Sokoine iendelee na kuwanufaisha wakulima kuongeza tija na uzalishaji  kwa kudhibiti visumbufu vya mazao yake. “ alisema Kusaya ,Kwa mujibu wa takwimu za wizara ya kilimo kuwa uzalishaji wa ndani wa mbegu bora umefikia tani 61,703 mwaka 2019

Kwa upande wake Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Kilimo Sokoine Prof,Raphael Chibunda alimshukuru Katibu Mkuu huyo kwa kutembelea chuo hicho na kuwa wapo tayari kuanzisha mafunzo maalum ya muda mfupi kwa ajili ya kufundisha wataalam waliopo kazini na wale wanaopenda kujifunza kilimo cha kisasa.

Prof.Chibunda alisema SUA itaendeleza ushirikiano na Wizara ya Kilimo kupitia taasisi za utafiti wa Kilimo (TARI) na kampuni ya mbegu nchini (ASA) na Taasisi ya Udhibiti wa Mbegu Tanzaia (TOSCI) kuzalisha mbegu bora za mazao  kwa kutumia teknolojia na wataalam waliopo nchini.

“SUA ina msitu wa wataalam hivyo tunaahidi tutashirikiana na wizara ya kilimo kufanya tafiti za mbegu bora na pia kuzalisha mbegu hizo kwa matumizi ya ndani na nje ya nchi. ” alisitiza Prof.Chibunda

Aliongeza kusema kina mkakati wa kuanzisha digrii maalum itakayosaidia kuzalisha wataalam wabobezi kwenye usimamizi wa sekta ya ushirika na kilimo nchini ili kuunga mkono jitahada za serikali kuwa na ushirika imara.

Katika hatua nyingine Prof.Chibunda aliomba Serikali iweke utaratibu wa kuratibu waduka ya pembejeo ili yawe na wataalam waliosomea kilimo na mifugo kwa ajili ya kutoa huduma za ushauri kwa wakulima.

Katibu Mkuu huyo wa wizara ya Kilimo alisema lengo la wizara yake ni kuhakikisha kunakuwepo sera nzuri na mazingira wezeshi ya kufanya kilimo kuwa ajira, uchumi na biashara kwa watanzania walio wengi.
Share:

0 comments:

Post a Comment

Copyright © WAZO HURU | Powered by Blogger Design by ronangelo | Blogger Theme by NewBloggerThemes.com