METDO Tanzania

METDO Tanzania

Tuesday, March 17, 2020

SIMIYU YAFUNGA KAMBI YA KITAALUMA TAHADHARI DHIDI YA CORONA

Katibu Tawala wa Mkoa wa Simiyu, Bw. Jumanne Sagini akizungumza na wanafunzi wa Kidato cha Sita mkoani humo, kabla ya kufunga kambi ya kitaaluma kwa wanafunzi hao   ambayo ilikuwa ikiendelea katika Shule ya Sekondari ya Wasichana Maswa, kwa lengo la kuchukua tahadhari dhidi ya Corona.

Baadhi ya wanafunzi wa kidato cha Sita wakimsikiliza Katibu Tawala wa Mkoa wa Simiyu, Bw. Jumanne Sagini(hayupo pichani) akizungumza na wanafunzi wa Kidato cha Sita mkoani humo, kabla ya kufunga kambi ya kitaaluma kwa wanafunzi hao  ambayo ilikuwa ikiendelea katika Shule ya Sekondari ya Wasichana Maswa kwa lengo la kuchukua tahadhari dhidi ya Corona.
Afisa Afya wa Mkoa wa Simiyu, Bw. Reuben Malimi akitoa elimu ya tahadhari dhidi ya Homa ya Mapafu inayosababishwa na Virusi vya Korona kwa wanafunzi wa kidato cha Sita mkoani humo waliokuwa katika kambi ya Kitaaluma shule ya Sekondari ya Wasichana ya Maswa, kabla ya kambi hiyo kufungwa ili kuchukua tahadhari dhidi ya Corona.

Baadhi ya wanafunzi wa kidato cha Sita wakimsikiliza Katibu Tawala wa Mkoa wa Simiyu, Bw. Jumanne Sagini(hayupo pichani) akizungumza na wanafunzi wa Kidato cha Sita mkoani humo, kabla ya kufunga kambi ya kitaaluma kwa wanafunzi hao ambayo ilikuwa ikiendelea katika Shule ya Sekondari ya Wasichana Maswa kwa lengo la kuchukua tahadhari dhidi ya Corona.

Afisa Elimu wa Mkoa wa Simiyu, Mwl. Ernest Hinju akitoa taarifa ya hali ya kambi ya kitaaluma kwa waanfunzi wa kidato cha sita mkoani humo, kabla ya kumkaribisha Katibu Tawala wa Mkoa wa Simiyu, Bw. Jumanne Sagini kuzungumza na wanafunzi hao, kabla ya kufunga kambi ya kitaaluma kwa wanafunzi hao ,  ambayo ilikuwa ikiendelea katika Shule ya Sekondari ya Wasichana Maswa, kwa lengo la kuchukua tahadhari dhidi ya Corona.

Uongozi wa Mkoa wa Simiyu umefunga kambi ya Kitaaluma kwa wanafunzi wa kidato cha Sita mwaka 2020 iliyokuwa ikifanyika katika Shule ya Sekondari ya Wasichana Maswa , ikiwa ni sehemu ya tahadhari dhidi ya Homa kali ya Mapafu inayosababishwa na Virusi vya Corona.


Akifunga kambi hiyo, Machi 16, 2020  Katibu Tawala wa Mkoa wa Simiyu, Bw. Jumanne Sagini amesema uongozi wa mkoa umefikia hatua hiyo kuchukua tahadhari kama ilivyoelekezwa na viongozi mbalimbali wa Kitaifa juu ya kuzuia mikusanyiko ya watu wengi isiyo ya lazima katika kipindi hiki ambacho kumeripotiwa idadi ya watu kadhaa kubainika kuwa na virusi vya Corona katika nchi mbalimbali.

“Kutokana na Maelekezo ya Serikali Mkoa umeona kambi hii ifungwe kwa ajili ya tahadhari dhidi ya Corona,  Mhe. Rais amesitisha mbio za Mwenge wa Uhuru kwa mwaka 2020, Mhe. Waziri Jafo amesitisha UMISETA na UMITASHUMTA na tahadhari mbalimbali zimeendelea kutolewa na Serikali ikiwemo ya kuzuia mikusanyiko; sisi hapa tuna wanafunzi  takribani 1000 kutoka shule 10 hivyo tumekubaliana kwa pamoja tuifunge kambi hii,” alisema Sagini.

Aidha, Sagini amesema pamoja na kambi za kitaaluma kufungwa Mkoa utaendelea kusimamia utekelezaji wa mkakati wa taaluma wa mkoa ili walimu, wanafunzi na wadau wengine wa elimu waweze kutimiza wajibu wao kuhakikisha Mkoa unatimiza adhma yake ya kuwa miongoni mwa mikoa itakayofanya vizuri katika mitihani yote ya Kitaifa.

Kwa upande wake Afisa Elimu wa Mkoa wa Simiyu, Mwl. Ernest Hinju amesema wanafunzi hao walitakiwa kukaa kambini muda wa wiki sita kwa ajili ya maandalizi ya Mtihani wa Taifa unaotarajiwa kufanyika mwezi Mei 2020, hivyo pamoja na kusitisha kambi hiyo walimu wamehimizwa kutimiza wajibu wao katika ufundishaji na wanafunzi wametakiwa kwenda kusoma kwa bidii ili kufikia lengo la Mkoa.

Awali akitoa elimu ya ugonjwa wa homa ya mapafu unaosababishwa na virusi vya Corona kwa wanafunzi na walimu kabla ya kambi kufungwa, Afisa Afya wa Mkoa wa Simiyu, Bw. Reuben Malimi amesema ugonjwa huo hauna tiba matibabu yanayofanyika yanazingatia dalili zinazoonekana kwa mgonjwa, hivyo ni vema kila mmoja  akachukua tahadhari kwa kuzingatia maelekezo na elimu inayotolewa na wataalamu wa afya katika maeneo mbalimbali.

Nao wanafunzi wa Kidato cha Sita wa Mkoa wa Simiyu wameshukuru uongozi wa Mkoa kuchukua tahadhari dhidi ya Virusi vya Corona kwa kutoa elimu kuhusu Corona  kabla ya kufunga kambi, huku wakieleza namna ambavyo kufungwa kwa kambi kunaweza kuathiri malengo yao waliyojiwekea.

“Tunashukuru uongozi wa Mkoa kutoa elimu  na kuchukua tahadhari ya Corona kwa kufunga kambi ni hatua ya kutuhakikishia usalama, lakini kambi ilitusaidia kujua namna ya kujibu maswali ya mtihani wa Taifa na kujifunza mada ngumu tulizoshindwa shuleni kupitia kwa walimu mahiri, tutatumia muda huu kujisomea kwa bidii ili tufaulu vizuri mtihani wa Taifa,” alisema Isack Ndassa kutoka Shule ya Sekondari Kanadi Itilima.
Share:

0 comments:

Post a Comment

Copyright © WAZO HURU | Powered by Blogger Design by ronangelo | Blogger Theme by NewBloggerThemes.com