METDO Tanzania

METDO Tanzania

Tuesday, March 10, 2020

MHE,MAVUNDE AWATAKA VIJANA KUTOKATA TAMAA, WACHANGAMKIE FURSA



Zaidi Vijana 20,000 watanufaika na soko la mazao ya matunda nchini kote katika viwanda vilivyopo hapa nchini ikiwemo cha Bakharesa ambapo yatatumika katika utengenezaji wa sharobati (Juice), hivyo kuwataka vijana hao kutokata tamaa.

Akiongea wakati wa ufunguzi wa kongamano la vijana wakulima lililofanyika katika ukumbi wa Kanisa Katoliki uliopo wilayani Butiama mkoa wa Mara Naibu Waziri Ofisi ya Waziri mkuu vijana Kazi na Ajira Mhe. Antony Mavunde amesema mazungumzo yamefanyika baina ya Wizara yake na uongozi wa kiwanda cha Bakharesa ili aweze kununua matunda kama maembe na ukwaju yanayozalishwa na vikundi vya vijana.

Amewataka vijana kutokata tamaa na kuwataka kujiajiri katika fursa walizonazo zikiwemo ardhi ya kilimo nguvu na afya bora walizobarikiwa kwa kuwa tayari Serikali imeshaweka mazingira wezeshi kwa vijana kufanya kazi hiyo.

Amewataka vijana hao kutumia kongamano hilo la siku mbili ili kupata mbinu mpya na fursa za kilimo ufugaji na uvuvi ili kuweza kuongeza uzalishaji wa mazao ya kilimo,mifugo na uvuvi.

Aidha amesema kwamba ili kuhakikisha vijana wanapata mbinu bora na wanashiriki kikamilifu katika kilimo na Ofisi ya Waziri Mkuu inaendesha programu ya kuwapatia vijana ujuzi wa kilimo cha kisasa kwa kutumia teknolojia ya Kitalu Nyumba (Green House).

Mhe. Mavunde amebainisha kwamba Programu hii inalenga kuzifikia Halmashauri zote nchini ambapo zaidi ya vijana 18,800 watanufaika na mafunzo ya kilimo kupitia teknolojia hii ambapo jumla ya vijana 8,700 kutoka Halmashauri 84 za Mikoa 12 tayari wamepatiwa mafunzo ya kilimo
kupitia teknolojia hiyo.

Hata hivyo amebainisha kwamba zaidi ya Shilingi Bilioni 4.06 zimetolewa katika vikundi vya vijana 732. Kwa ajili ya kufanya ujasiriamali ambapo vijana wameweza kupata mitaji kwa ajili ya miradi ya Kilimo cha kibiashara.

Mhe. Mavunde amezitaka Halmashauri zote kutenga maeneo rafiki ya kilimo kwa ajili ya vijana kwa kuwa lilikuwa azimio la Wakuu wa Mikoa la mwaka 2014 kuhusu kukabiliana na ukosefu wa ajira kwa vijana.

Akihutubia vijana hao amewataka kutumia fursa ya mikopo kupitia Mfuko wa Maendeleo ya Vijana na fedha za mikopo zilizotengwa kutokana na mapato ya ndani (4-4-2) kwa ajili ya kuanzisha miradi ya kilimo mifugo na uvuvi na kuwasihi kurudisha fecha hizo kwa wakati ili vijana wengine wanufaike.

Kwa upande mwingine Mhe. Mavinde awataka maafisa ugani Wadau wa Kilimo kuwasaidia vijana kwa kuwapatia utaalamu na mbinu bora za kisasa katika kilimo mifugo na uvuvi.

Awali Mkuu wa Mkoa wa Mara Mhe. Adamu Malima akimkaribisha Naibu waziri huyo amewataka Wadau kuwawezesha vijana kutumia teknolojia ya habari hasa mitandao ya kijamii kuwawezesha vijana kupata habari zinazofaa kuhusu kilimo

Amesema teknolojia hii ikitumika vyema itawezesha kuwafanya vijana wavutiwe na kilimo na kuondoa taswira iliyojengaka kuwa kilimo ni mambo ya kizamani.
Share:

0 comments:

Post a Comment

Copyright © WAZO HURU | Powered by Blogger Design by ronangelo | Blogger Theme by NewBloggerThemes.com