METDO Tanzania

METDO Tanzania

Wednesday, December 11, 2019

SAME TEACHERS SACCOS CHAWAUNGANISHA WAFANYAKAZI WA SERIKALI WILAYANI SAME


Mwenyekiti wa Tume ya Maendeleo ya Ushirika Tanzania Dkt. Titus Kamani, akizungumza na viongozi wa Chama cha Akiba na Mikopo cha Walimu Same (Same Teachers SACCOS).
Mrajis Msaidizi wa Vyama vya Ushirika mkoa wa Kilimanjaro, John Henjewele akizungmza wakati wa Kikao cha Mwenyekiti wa Tume ya Maendeleo ya Ushirika Tanzania Dkt. Titus Kamani, na Wajumbe wa Bodi ya Chama cha Akiba na Mikopo cha Walimu Same (Same Teachers SACCOS).
Mwenyekiti wa Tume ya Maendeleo ya Ushirika Tanzania Dkt. Titus Kamani, (Wa nne kutoka kulia)  akiwa katika picha ya pamoja na Wajumbe wa Bodi ya Chama cha Akiba na Mikopo cha Walimu Same (Same Teachers SACCOS).
Mwenyekiti wa Tume ya Maendeleo ya Ushirika Tanzania Dkt. Titus Kamani, (Wa nne kutoka kulia)  akiwa katika picha ya pamoja na Watendaji wa Chama cha Akiba na Mikopo cha Walimu Same (Same Teachers SACCOS).

Chama cha Akiba na Mikopo cha Walimu Same (Same Teachers SACCOS), kinaunganisha wafanyakazi wa Serikali wilaya ya Same ambacho kilianzishwa na wanaushirika walimu na baadaye walikubaliana kufungua wigo wa kupokea wafanyakazi toka Idara nyingine ambao kwa sasa fungamano lao ni wafanyakazi wa serikali wilaya ya Same.

Same Teachers SACCOS kimejiendeleza na kujiimarisha kwa kukuza mtaji wake wa ndani kufikia Shilingi Bilioni moja na milioni mia saba (1.7 Bilioni) na kuongeza idadi ya wanachama kwa kila mwaka ambapo kufikia tarehe 30/09/2019 chama kina idadi ya wanachama 1,533 (wanaume 764 na wanawake 769). Idadi hii ya wanachama inajumuisha wanachama waliopo kazini, waliostaafu na waliohama ambao hawajachukua hisa zao.

Taarifa ya Same Teachers SACCOS iliyosomwa na Mwenyekiti wa Bodi, Mwalimu Omari Mchome, kwa Mwenyekiti wa Tume ya Maendeleo ya Ushirika Tanzania Dkt. Titus Kamani, ilionyesha kuwa chama hicho kimefanikiwa kutoa huduma za kifedha kwa wanachama kama vile (ukusanyaji wa hisa, Akiba, Amana na Viingilio) na utoaji wa mikopo mbalimbali ili kuwawezesha wanachama wake  kiuchumi.

“Chama cha Akiba na Mikopo cha Walimu Same kimefanikisha ustawi wa jamii hasa elimu, makazi bora, biashara kilimo na miradi mingine mbalimbali hatimaye kupunguza umaskini kwa wanachama wake kwa kiasi kikubwa. Chama kimekuwa kikitoa elimu kila mwaka ili kupata ufahamu zaidi juu ya ushirika na Asasi nyingine za fedha,” alisema Mwalimu Mchome.

Dkt. Kamani alifanya ziara ya kikazi hivi karibuni mkoani Kilimanjaro kujionea maendeleo na changamoto za vyama vya ushirika ambapo akiwa wilayani Same amewapongeza Walimu na Watumishi wengine wa wilaya hiyo kuanzisha na kusimamia vizuri SACCOS yao ambayo imepata mafanikio makubwa.

“Nawapongeza Walimu kwa kuanzisha na kusimamia vizuri SACCOS yenu  na kupata mafanikio makubwa; ningeshangaa kama SACCOS ya Walimu ambao ni Wataalam tunaowategemea kama kioo cha jamii, mngeshindwa kuwaleta watumishi pamoja na kupata suluhisho la mtaji,” alisema Mwenyekiti wa Tume ya Ushirika.

Jumla ya mikopo yote iliyotolewa na Same Teachers SACCOS tangu chama kianzishwe hadi kufikia tarehe 30 Septemba 2019 ni shilingi bilioni kumi na tano, milioni mia tisa thelathini na tatu laki saba ishrini na saba mia nane arobaini na tano (15,933,727,845/). Mikopo hii inalenga kuwakwamua wanachama katika shughuli mbalimbali kama vile Kilimo na Ufugaji, malipo ya Ada za shule kwa watoto na wao wanapokwenda kujiendeleza, Ujenzi, Biashara, Ununuzi wa vyombo vya usafiri, na kutatua matatizo ya kijamii kama kusaidia kipindi cha ugonjwa.

Aidha, Chama hiki kimeweza kutoa misaada kwa jamii inayowazunguka kwa kipindi cha miaka miwili mfululizo ambapo kimetoa vifaa viwili vya kusaidia kupumua (oxygen flow metre), shuka 200 na blanketi 200 kwa hospitali ya wilaya ya Same.
Share:

0 comments:

Post a Comment

Copyright © WAZO HURU | Powered by Blogger Design by ronangelo | Blogger Theme by NewBloggerThemes.com