METDO Tanzania

METDO Tanzania

Thursday, October 10, 2019

MAONYESHO YA SIKU YA CHAKULA DUNIANI KITAIFA MKOANI SINGIDA YAANZA KWA KISHINDO





Na Innocent Natai, Singida

Mkuu wa mkoa wa Singida Dkt Rehema Nchimbi amewataka wakazi wa mkoa wa Singida na mikoa mingine kujitokeza kwa wingi katika maadhimisho ya siku ya chakula duniani yanayofanyikia kitaifa mkoani Singida ili kupata elimu ya lishe bora na kilimo chenye tija ili kuepukana na njaa kitaifa na Dunia kwa ujumla.

Ameyasema hayo leo tarehe 10 Octoba 2019 alipotembelea kukagua maandalizi ya maadhimisho hayo yaliyoanza rasmi katika viwanja vya Bombadia (Peoples) ambapo ndipo maonyesho hayo yanapofanyikia.

Nchimbi amewataka wakazi wa singida kuiona fursa waliyoipata ya maonyesho hayo kupangwa kufanyikia mkoani hapo na kuitumia kwa kutembelea mabanda kwa ajili ya kupata elimu ya  afya na lishe bora kwa ujumla na kujionea fursa zilizopo katika kilimo pia.

Amesem kuwa endapo watatembelea watapata fursa ya kujionea vyakula lishe na kujifunza namna bora ya kuandaaa na kulima mazao lishe ili kuepukana na njaa katika jamiii yao na kwa dunia kwa ujumla.

“Unapopata fursa ya kuja au kusikia taarifa hizi hakikisha unamjulisha na mwenzako kwani hii ni fursa kubwa sana nina imani hapa pia wajasiriliami wadogo wadogo  kupitia maonyesho haya watapata elimu na  fursa ya kuuza bidhaa zao’’ Alisema Dkt Nchimbi.

Akizungumzia hali ya maandalizi ya maonyesho hayo amesema kuwa mpaka sasa maandalizi yamekamilika na  muitikio ni mkubwa kwa wananchi wa mkoa wa Singida na mikoa ya jirani kwani kwa siku ya kwanza tu wananchi wameonyesha kuvutiwa na maonyesho hayo kwa kujitokeza kwa wingi katika viwanja hivyo.

Maonyesho hayo ya siku ya chakula Duniani kitaifa mkoani Singida  yameanza leo tarehe 10 Octoba 2019 na yanatarajiwa kuzinduliwa rasmi tarehe 12 Octoba 2019 na kuhitimishwa tarehe 16 Octoba 2019 ambapo ndio siku ya kilele.

Mgeni rasmi wakati wa kilele cha maadhimisho hayo anatarajiwa kuwa  Waziri wa Kilimo Mhe Japhet Hasunga (Mb) yakiwa na kaulimbiu ya “lishe bora kwa ulimwengu usio na njaa’’

MWISHO
Share:

0 comments:

Post a Comment

Copyright © WAZO HURU | Powered by Blogger Design by ronangelo | Blogger Theme by NewBloggerThemes.com