METDO Tanzania

METDO Tanzania

Tuesday, July 23, 2019

WAPUUZENI HAO WANAOTAKA KUKIVURUGA CHAMA CHETU-DK.BASHIRU

Na.Alex Sonna,Dodoma

Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Taifa, Dkt. Bashiru Ally,leo  ametoa wito kwa wanachama wa chama hicho kuwapuuza wale watu wanaoendeleza mjadala usiokuwa na tija ndani ya chama hicho, na akawahakikishia kwamba chama hicho kiko imara. Dk. Bashiru  ameyasema hayo wakati akitoa pongezi kwa hatua ya wanaCCM Mkoa wa Dodoma, kutaka Kanali Abdulrahman Kinana na Yusuf Makamba, makatibu wastaafu wa CCM kuchukuliwa hatua.
Hii ni baada ya makatibu hao wastaafu wiki iliyopita, kumwandikia barua Pius Msekwa, Katibu wa Baraza la Viongozi Wastaafu wa CCM wakilalamikia kuchafuliwa na Cryspian Musiba, anayejitambulisha kuwa mtetezi wa Rais John Magufuli.
Kwenye barua hiyo, Makamba na Kinana wamelalamika kuchafuliwa na kuzushiwa huku wakidai  serikali imeshindwa kuchukua hatua. Hata hivyo, wamehoji ‘ulinzi’ anaopewa Mtu huyo  anayewachafua.

“Wapuuzeni, hatuogopi kukosolewa, lakini hatuko tayari kudharauliwa, kutukanwa na kubezwa na majina yaliyo na kebehi na watu wasio na shukrani. Hatujafunzwa hivyo, hatujazoea hivyo,” amesema Dk.Bashiri bila kutaja jina lolote.
Aidha, Dk. Bashiru amesema, uongozi wa CCM hautaruhusu malumbano ndani ya chama hicho, huku akieleza kwamba mwenyekiti wake, Dk. Magufuli yuko tayari kuwasamehe, ili kukijenga chama.
“Msijifanye majasiri wa kupambana na malumbano, hakuna ruksa hiyo kwenye chama chetu. Waacheni waseme watachoka wenyewe.
“Ole wake mwanaCCM yeyote atakayetaka kutumia fursa ya malumbano hayo kutafuta kiki, ya kisisasa ili achaguliwe kwenye Serikali za mtaa, hapana msifanye hivyo.
 “Jifunzeni kutoka kwa kiongozi wetu ambaye wakati wote hana muda wa malumbano. Amevumilia, wanaomtusi wengine wana umri wa watoto wake amewavumilia na yuko tayari kuwasamehe pia.  Lakini kwa kufanya hivyo si kwamba ni muoga.
“Mwalimu Julius Nyerere alishatuasa tujisahihishe, kujisahihisha ni kujiimarisha, tujikosoe, tukosoane kwa adabu kwa nidhamu tuache utoto.Kisiwe chama cha siasa za kipuuzi, sababu majira haya ni ya uchaguzi,” amesema Dk. Bashiru.

Share:

0 comments:

Post a Comment

Copyright © WAZO HURU | Powered by Blogger Design by ronangelo | Blogger Theme by NewBloggerThemes.com