METDO Tanzania

METDO Tanzania

Monday, July 29, 2019

TIMU YA WATAALAMU YA TAASISI YA KUENDELEZA KILIMO AFRIKA (AGRA) YAKUTANA NA VIONGOZI WA WIZARA YA KILIMO KUJADILI UZALISHAJI NA TIJA KATIKA MAZAO YA KILIMO NA UONGEZAJI THAMANI


Timu ya wataalam kutoka katika Taasisi ya kuendeleza kilimo Afrika (AGRA) imekutana na viongozi wa wizara ya kilimo na wizara ya Viwanda na Biashara lengo likiwa ni kuajadiliana  namna ya  kuongeza uzalishaji na tija katika mazao ya kilimo  pamoja na uongezaji wa thamani wa mazao hayo.

Mkutano huo ambao umehudhuriwa na Waziri wa Viwanda na Biashara Mhe. Innocent Bashungwa, Naibu waziri wa Kilimo Mhe Omary Mgumba na Naibu Waziri kilimo Mhe. Hussein Bashe, pamoja na Rais wa AGRA Afrika Dkt. Agnes Kalibata umefanyika tarehe 29.07.2019 katika ukumbi wa mikutano wa kilimo IV mjini Dodoma ambapo wamekubaliana.

Kuimarisha uzalishaji wa mazao manne ambayo,ni alizeti, mahindi, mpunga pamoja na maharage ya soya ambayo yanahuitaji mkubwa katika soko.

Akizungumza katika kikao kazi hicho Rais wa AGRA Dkt. Agnes Kalibata  amesema kwamba  Tanzania inaweza kuwa ghala la chakula afrika endapo  itaendea kuwekeza kikamilifu katika sekta ya mbegu hapa nchini kwa kuwa wakulima wengi hawatumii mbegu bora za kilimo.

Akizungumza katika mkutano huo Dkt. Kalibata  amesema wakati umefika kuongeza uwekezaji katika sekta ya mbegu kwa kuimarisha miundombinu ya umwagiliaji  katika mashamba ya mbegu ili ziweze kuzalishwa kwa uhakika na kuongeza tija kwa wakulima.

Hata hivyo ameshauri wizara ya kilimo kuandaa jukwaa maalum la wazalishaji wa mbegu (Seed Platform) ambalo litasaidia kuongeza uhusiano baina ya wazalishaji wa mbegu wa serikalini na wa sekta binafsi katika kusaidia ukuaji wa viwanda hapa nchini.

"Tanzania ina viashiria vingi vinavyoweza kusaidia ukuaji wa viwanda vya kilimo Kama wataongeza kiasi cha uzalishaji mbegu, kuongeza idadi ya wauzaji pembejeo za kilimo (Agro- Dealer), kuimarisha huduma za ugani kwa wakulima na kuongeza usajili wa makampuni ya mbegu" Alisema Dkt. Kalibata

Aidha mwenyekiti wa kikao hicho ambaye ni waziri wa viwanda na biashara Mhe. Innocent Bashungwa amesema wamekubalina na AGRA Kuweka mikakati madhubuti  ya kuendeleza mazao ya mafuta ili kupunguza uagizaji wa bidhaa hiyo nje ya nchi.

Hata hivyo   Mhe. Bashungwa  amesisitiza kwamba AGRA isaidie katika kuongeza uzalishaji wa mbegu hapa nchini ambapo uzalishaji huo  utasaidia kuongeza malighafi za viwanda hapa nchini.

Akitolea mfano viwanda vya alizeti Mhe. Bashungwa amesema kwamba  hapa nchini kuna viwanda vya kusindika alizeti vipatavyo 29 lakini vyote vinazalisha chini ya asilimia 30 kwa kukosa malighafi za viwandani.

Mhe. Bashugwa aliendea kumfafanulia Rais wa AGRA Afrika kwamba nchi zinazoizunguka tanzania zinauhitaji mkubwa wa mazao kama soya,mahindi,alizeti  mpunga na Degu  hivyo kwa ushirikiano huo utasaidia sana katika upatikanaji wa soko kwa wakulima wetu.

Akiongea kwa niaba ya serika Naibu Waziri Mh. Mgumba amesema makubaliano hayo yamelenga kuongeza tija na uzalishaji kwa wakulima na kuongeza ushindani  katika soko kuwa na bei nzuri kwa wanunuzi.

Hata hivyo Mhe. Mgumba ameeleza kwamba  wakuima wanatakiwa kulima kulingana na mahitaji ya soko  na kutokana na makubaliano hayo kutasaidia wakulima kupunguza gharama za uzalishaji  hivyo kusaidia kupungua bei za mazao  ikilinganishwa na hali  ilivyo sasa.

Aidha, wamekubaliana kuimarisha   sekta binafsi  hususani katika uzalishaji wa mbegu, huduma za ugani na kuijengea mazingira mazuri ili kuweza kuongeza uzalishaji , na kutoa ajira kwa watanzania kwa kupunguza gharama za uwekezaji

Naye Mh Naibu Waziri wa Kilimo Hussein Bashe amesema wakulima wanakabiliwa na changamoto kubwa ya kiwango  kidogo cha uzalishaji katika ekari na gharama kubwa ya uzalishaji hivyo kuwashauri AGRA kuangalia namna ya kuwasaidia wakulima kupunguza gharama ya uzalishaji na kuongeza kipato.

Kwa upande mwingine Naibu waziri Bashe amewaomba AGRA kusaidia uzalishaji wa mbegu hapa nchini, ili ziweze kupatikana kwa gharama ndogo  na mkulima kupata matokeo chanya.

Katika kuimarisha ufuatiliaji wa shughuli za kilimo wamekubaliana kuhusu fedha zinazotoka kwa wafadhili zijulikane kila  zinapokwenda ili kuhakikisha lengo lilikusudiwa linafikia alisema Mhe. Bashe

MWISHO
Share:

Related Posts:

0 comments:

Post a Comment

Copyright © 2025 WAZO HURU | Powered by Blogger Design by ronangelo | Blogger Theme by NewBloggerThemes.com