METDO Tanzania

METDO Tanzania

Sunday, June 2, 2019

MTATURU AWEZESHA UPATIKANAJI WA MIL 7.4 KWA AJILI YA UNUNUZI WA VIFAA VYA KWAYA YA JERUSALEM




MKUU wa Wilaya ya Ikungi Mh Miraji Mtaturu ameshiriki harambee na kuchangia shilingi milioni 4.6 kwa ajili ya ununuzi wa vifaa vya kwaya ya New Jerusalem ya Kanisa FPCT Mbughantigha-Matongo lililopo wilayani humo.

Aidha kupitia harambee hiyo amewezesha kupatikana jumla ya shilingi milioni 7.4 DC 

Akizungumza katika harambee hiyo mh Mtaturu amewaomba waumini kuendelea kuilinda amani ya nchi kwa kuwa bila ya kuwepo kwa amani jambo lolote la kimaendeleo ikiwemo kuabudu halitaweza kufanyika.

“Tumejumuika hapa kwa sababu tuna amani,bila ya kuwa na amani tusingekuwepo hapa na kufanikisha jambo hili la Mungu,niwashukuru sana Kanisa kwa kunialika kwenye jambo hili muhimu,kwani vyombo hivi tunavyotafuta leo vitaenda kupeleka neno la Mungu kwa waumini na wao  wakimjua  Mungu watakuwa Raia wema na hivyo watadumisha amani,

“Serikali yetu ya awamu ya tano chini ya Rais wetu mpendwa Mhe. Dkt John Pombe Magufuli inatambua na kuthamini sana mchango wa Taasisi za Dini kwenye huduma mbalimbali za kijamii sambamba na kudumisha amani,na imeendelea kuboresha huduma za kijamii kama Elimu,Afya,na Miundombinu ili kuharakisha maendeleo ya nchi yetu”alisema mh Mtaturu.

Amesema ushahidi wa hilo ni katika wilaya hiyo ambapo kwenye kitongoji cha Mbughantigha mwaka jana serikali imepeleka shilingi milioni 66.5 ili kujenga madarasa mawili na ofisi ya mwalimu,matundu manne ya vyoo kwa ajili ya shule shikizi ambayo imeondoa tatizo la watoto wadogo waliokuwa wanatembea km 14 kufuata shule ya msingi Matongo.

“Mbali na hilo serikali yetu pia imeleta shilingi milioni 187.5  kwa ajili ya umaliziaji wa maboma ya madarasa14 ya shule 7 za sekondari na shilingi milioni 127  kwa ajili ya kujenga vyumba vya madarasa ya shule za msingi pamoja na utengenezaji wa madawati,na kila mwezi wilaya tunapokea shilingi milioni 103 kupitia mpango wa elimu bila malipo maarufu kama Elimu Bure,”aliongeza mh Mtaturu.

Amewapongeza wananchi kwa kuanzisha  ujenzi wa madarasa mengine mawili na ofisi ambayo yamefikia usawa wa madirisha na kuwahakikishia kuwa serikali itaendelea kuwaunga mkono ili watimize dhamira ya kujenga madarasa ya kutosha na kufungua shule mpya ya msingi Mbughantigha.

Mchungaji kiongozi wa kanisa hilo John Matheo amemshukuru Mkuu wa Wilaya kwa upendo wake wa kukubali kuja kushirikiana nao na kusema wanabarikiwa sana kuwa na viongozi wa serikali wanaowajali watu wao.

Akisoma risala ya kwaya Mwalimu Mary Lengalenga amesema kwaya hiyo ilianzishwa mwaka 2014 ikiwa na wanakwaya 6 na inahitaji shilingi milioni 13 ili kukabiliana na  upungufu wa vyombo vya uinjilishaji kupitia nyimbo.

Mh Mtaturu akiongozana na viongozi wa Kijiji,Kata na Tarafa ya Ikungi  wametumia shughuli hiyo pia kukagua ujenzi wa shule  ili kuona kazi zinazoendelea.

"Ikungi Yetu Sote Tuijenge Pamoja"
Share:

0 comments:

Post a Comment

Copyright © WAZO HURU | Powered by Blogger Design by ronangelo | Blogger Theme by NewBloggerThemes.com