METDO Tanzania

METDO Tanzania

Saturday, October 20, 2018

Hakuna cha msalia mtume usipotekeleza sheria- Profesa Kikula





Na: Rhoda James - Singida

Mwenyekiti wa Tume ya madini, Profesa Idris Kikula amesema kutokujua sheria ya madini si kigezo wala sababu ya kukwepa adhabu ya ukiukwaji wa sheria hiyo na kuwataka wachimbaji wa madini kuzingatia na kufuata sheria na taratibu za kujihusisha na biashara hiyo.

Ameyasema hayo jana tarehe 16 October 2018 mkoani Singida alipokuwa katika  kikao na Mkuu wa Mkoa wa Singida, Rehema Nchimbi, Kamati ya ulinzi na usalama ya mkoa huo, viongozi wa wachimbaji wadogo pamoja na baadhi ya wachimbaji wadogo wa Jasi na madini ya dhahabu.

Profesa Kikula ameeleza kuwa, kazi ya tume ni pamoja na kutoa elimu kwa wachimbaji wa madini, Hii ni sababu kubwa ya kuwatembelea siku hii ya leo, “tumewatembelea ili kuwafundisha na kuwakubusha kuhusu sheria zilizopo pamoja na marekebisho ya sheria ya madini ya mwaka 2017”. 

Tunapita ili kutoa elimu katika masuala mbalimbali ikiwa ni pamoja na masuala ya kutuza kumbukumbu, mazingira na usalama migodini, utoaji wa tozo mbalimbali kwa mujibu wa sheria ili tutakapokuja tena awamu nyingine na kukuta mmekiuka taratibu sheria ichukue mkondo wake.

Aidha, Profesa Kikula amewataka wachimbaji wadogo, wa kati na hata wakubwa nchini kuhakikisha kuwa wanakaa pamoja na uongozi wa  wilaya au mkoa husika ili kukubaliana juu ya namna ya uwajibikaji katika kutoa huduma kwa jamii (CSR). 

“Mikataba hii mnayoingia itasaidia kujua ni kiasi gani mnapata, kiasi gani unatakiwa kulipa kuligana na unachokipata ili Serikali ipate stahiki zake. Alisema Profesa Kikula.

Pamoja na hayo,  Profesa Kikula amewasihi viongozi wa wachimbaji wadogo (REMA) kuhakikisha wanashirikiana kwa karibu  na wachimbaji wadogo ili kuhakikisha kuwa wachimbaji hao wanajiunga katika vikundi na kuvirasimisha ili Serikali iwatambue na kuwapa huduma wanayostahili kwa wakati.

Akizungumza katika kikao hicho, Mkuu wa Mkoa wa Singida, Rehema Nchimbi, amewataka viongozi wa mkoa, wilaya, kata na hata vijiji kubadilika na kushiriki katika kutatua matatizo ya wananchi kwa karibu.

Aidha, amewataka , watumishi kujishughulisha kwa juhudi na kujituma pasipo kusubiri kuambiwa jambo la kufanya na badala yake wajifunze kufikiri jambo jema linalohitaji kufanyiwa kazi na kutekeleza kwa wakati ili kupunguza changamoto zinazojitokeza.

Akijibu swali la mchimbaji mdogo wa madini(Jina halikufahamika), aliyehoji  juu ya leseni ya utafiti kuchukua muda mrefu pasipo wananchi kupewa maelezo yoyote Kamishna wa Tume ya Madini Abudulkarim Mruma  alifafanua kuwa leseni ya utafiti inatolewa kwa awamu tatu ambapo awamu ya kwanza inachukua miaka minne, ya pili miaka mitatu na ya tatu miaka miwili kwa mujibu wa sheria ya madini na baada ya hapo kama mchimbaji hajapata chochote anarudisha eneo hilo kwa Serikali.
Share:

0 comments:

Post a Comment

Copyright © WAZO HURU | Powered by Blogger Design by ronangelo | Blogger Theme by NewBloggerThemes.com