METDO Tanzania

METDO Tanzania

Tuesday, July 10, 2018

Naibu Waziri wa Madini Doto Biteko afunga machimbo ya Epanko mkoani Morogoro

Naibu Waziri wa Madini Mhe Doto Mashaka Biteko
Katibu Mtendaji wa Tume ya Madini, Profesa Shukran Manya akiwasilisha taarifa ya uchunguzi wa shughuli za uchimbaji madini ya kinywe na vito katika machimbo ya Epanko mbele ya Naibu Waziri wa Madini, Dotto Biteko, Mkuu wa Wilaya ya Ulanga, Jackob Kassema pamoja na watendaji kutoka Wizara ya Madini (hawapo pichani) kwenye ofisi ya Mkuu wa wilaya UlangaKutoka kulia ni Naibu Waziri wa Madini, Doto Biteko, Katibu Mtendaji wa Tume ya Madini, Profesa Shukran Manya na Kamishna wa Madini kutoka Tume ya Madini Dkt. Athanas Macheyeki wakielekea kwenye machimbo ya Epanko yaliyopo katika wilaya ya Ulanga mkoani Morogoro

Na George Binagi, Morogoro

Naibu Waziri wa Madini Mhe Doto Mashaka Biteko ameagiza kusitishwa shughuli za uchimbaji madini katika machimbo ya Epanko iliyopo eneo la Mahenge katika Halmashauri ya Wilaya ya Ulanga mkoani Morogoro kutokana na machimbo hayo kukiuka kanuni na sheria za uendeshaji.

Naibu Waziri Biteko ametoa agizo hilo leo 10 Julai 2018 ametoa agizo hilo kufuatia ripoti ya timu maalumu aliyoiunda mwezi uliopita na Kamishina wa Madini nchini kuonyesha hakuna usimamizi na udhibiti mzuri wa madini ya vito aina ya Spinel, Green-Gernel pamoja na Ruby katika machimbo hayo na hivyo kuikosesha serikali mapato.

Mhe.Biteko ametoa muda wa siku tatu shughuli zote katika machimbo hayo ziwe zimesitishwa hadi pale taratibu zote za kisheria zitakapofuatwa ikiwemo wamiliki wote kuilipa serikali hasara itakayobainika kutokana na biashara ya madini hayo kufanyika kiholela huku akiongeza kwamba serikali inakusudia kuanzisha Ofisi ya Madini katika wilaya ya Ulanga itakayosimamia kwa karibu mwenendo wa shughuli za uchimbaji madini katika wilaya hiyo.

Ameagiza Kamati ya Ulinzi na Usalama ikiongozwa na Mkuu wa Wilaya Ulanga Mhe Jacob Kassema kuhakikisha hakuna kampuni inayoondoa mitambo yake katika eneo la Epanko kutokana na baadhi ya wachimbaji kutaka kuondoka eneo hilo kinyemela baada ya kubainika walikuwa wakifanya shughuli zao bila kufuata taratibu ikiwemo kutokuwa na leseni za uchimbaji.

Naye Katibu Mtendaji wa Tume ya Madini nchini, Profesa Shukrani Manya amesema baadhi ya wamiliki wa migodi katika machimbo ya Epanko wamekiuka taratibu kulingana na leseni za uchimbaji madini jambo ambalo serikali haiwezi kulivumilia na hivyo kuwataka wachimbaji wote kuhakikisha wanafuata taratibu zilizowekwa ili kufanya shughuli zao kihalali na kwamba watakaoshindwa kufanya hivyo watanyang’anywa leseni zao.

Mmoja wa wamiliki wa mgodi katika eneo la Epanko, Salim Hasham ambaye pia ni Mkurugenzi wa kampuni ya Ruby International amesema wako tayari kufuata taratibu zote huku akiiomba serikali kuwaruhusu kuendelea na shughuli za uchimbaji.

Itakumbukwa kwamba mwezi uliopita Naibu Waziri Biteko alifanya ziara katika machimbo ya Eponka na kubaini mapungufu kadhaa ikiwemo malalamiko kutoka kwa wananchi wa Kijiji cha Eponka wanaolalamika kudhulumiwa stahiki zao, utiririshaji ovyo wa maji taka katika mkondo wa mto Kilombero pamoja na uwepo wa usimamizi mbovu wa madini na hivyo kuisababishia serikali hasara kutokana na ukwepaji wa kodi na utoroshaji madini, hivyo Naibu waziri huyo wa madini kuagiza iundwe tume maalum ili kuchunguza uendeshaji wa biashara katika machimbo hayo.

Katika kutekeleza agizo hilo, Katibu Mtendaji Tume ya Madini nchini Profesa Shukurani Manya aliteua timu ya wataalamu sita ikiongozwa na Mwenyekiti Profesa Justinian Ikingura kutoka Chuo Kikuu cha Dar es salaam ili kufanya ukaguzi maalumu katika maeneo ya uchimbaji madini ya vito ikiwemo Spinel, Green-Gernel pamoja na Ruby na mradi tarajiwa wa madini ya Kinywe (Graphite) ambapo ripoti hiyo imeonyesha ukiukwaji wa taratibu za uchimbaji na biashara ya madini hayo. 

MWISHO.
Share:

0 comments:

Post a Comment

Copyright © WAZO HURU | Powered by Blogger Design by ronangelo | Blogger Theme by NewBloggerThemes.com