METDO Tanzania

METDO Tanzania

Sunday, November 5, 2017

MASAUNI APIGA MARUFUKU WANANCHI KUENDELEZA UJENZI GEREZA ISANGA, AITUNISHIA MISULI CDA DODOMA UVAMIZI ENEO MAGEREZA

maxresdefault
Na Mwandishi MOHA

NAIBU Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mhandisi Hamad Masauni amempa maelekezo Katibu Mkuu wa Wizara hiyo kuunda Kamati ya kuchunguza uvamizi wa viwanja vya Gereza Isanga uliofanywa na Mamlaka ya Ustawishaji Makao Makuu (CDA) mjini Dodoma.

Akizungumza mara baada ya kumaliza ziara yake ya kikazi katika Gereza hilo, Masauni alisema eneo hilo ambalo lina ukubwa wa ekari zaidi ya 150 lazima lirudishwe katika himaya ya Jeshi la Magereza kama lilivyokua awali.

“Eneo hili linalimilikiwa na Jeshi la Magereza tangu mwaka 1946, haiwezekani watu watokee na kuchukua ardhi hii kiholelaholela, hii haiwezekani hata kidogo, lazima uchunguzi ufanyike haraka iwezekanavyo na eneo lote lilrudi mikononi mwa jeshi,” alisema Masauni na kufafanua;

“Serikali ilishahamia hapa mjini Dodoma, hivyo shughuli za magereza zitaongezeka kwa kasi, na umuhimu wa maeneo utakua mkubwa zaidi kutokana na umuhimu wa jeshi hili katika kukuza uchumi.”

Aliongeza kuwa, jeshi hilo linahitaji kujenga nyumba za askari kwa kasi na kutokana na changamoto hiyo ya uvamizi uliofanywa ujenzi waweza kusuasua hivyo eneo hilo lahitajika kurudishwa haraka sana.

Masauni alifafanua kuwa, tayari amemuelekeza Katibu Mkuu wa wizara hiyo, Meja Jenerali, Projest Rwegasira kulichunguza suala hilo kwa kina kwa kuwa kuna taarifa ambazo bado hazijathibitishwa kuwa kati ya wamiliki wa viwanja hivyo walikua ni viongozi waandamizi wa CDA, Jeshi la Magereza pamoja na viongozi wakubwa mbalimbali.

Hata hivyo, Masauni alipiga marufuku mtu yeyote kuendeleza ujenzi wa eneo hilo hata kama ana vibali vyote vya kumiliki eneo.

Aidha, Mkuu wa Gereza Isanga, Keneth Mwambeje, akizungumzia suala hilo, alisema jeshi lake lina nyaraka  za mawasiliano kati ya viongozi wa gereza hilo ambao walikua kwa wakati huo pamoja na waCDA.

CDA ambayo ilivunjwa na Rais John Magufuli, ndio inahusika kugawa viwanja hivyo kwa wananchi zaidi ya mia moja ambao baadhi yao wamejenga na wengine wanaendelea na ujenzi katika eneo.
Share:

0 comments:

Post a Comment

Copyright © WAZO HURU | Powered by Blogger Design by ronangelo | Blogger Theme by NewBloggerThemes.com