METDO Tanzania

METDO Tanzania

Friday, August 5, 2016

MUFINDI YATEKELEZA AGIZO LA WAZIRI MKUU, YAKUSANYA MAPATO KWA ASILIMIA 82.7 2015-2016



Halmashauri ya wilaya ya Mufundi Mkoani Iringa imefanikiwa kutekeleza agizo la Waziri Mkuu wa Jamhuri ya muungano wa Tanzania katika ukusanyaji wa mapato ya ndani, baada ya kukusanya zaidi ya Shilingi Bilioni 4.7 sawa na asilimia 82.7 kati ya bilioni 5.6 ilizopanga kukusanya katika mwaka wa Fedha 2015-2016.

Taarifa ya kitengo cha habari na mawasilino cha halmashauri ya Wilaya ya Mufindi, imetanabaisha kuwa, mafanikio hayo yamebainishwa na Mwenyekiti wa halmashauri ya Wilaya ya Mufindi Mh. FESTO MGINA kwenye kikao cha kawaida cha baraza la madiwani wa halmashauri hiyo kilichoketi mjini Mafinga.


MGINA amesema, mafanikio hayo ni matokeo ya ufuatiliaji na usimamizi mzuri wa vyanzo vya mapato vya halmashauri kama vile mapato yatokanayo na usafirishaji wa mbao na Magogo, kuuzwa kwa sehemu ya msitu wa halmashauri sanjari na ushuru unaokusanywa kwa wafanyabiashara wadogo katika halmashauri hiyo.

Aidha, Mwenyekiti huyo ameongeza kuwa, pamoja na kutekeleza agizo la Waziri Mkuu la kila halmashauri kukusanya mapato kwa asilimia 80 na kuendelea, kikwazo kikubwa cha kutofikia asilimia 100 ni kuzaliwa kwa halmashauri ya mji wa Mafinga jambo amabalo lilisababisha kugawana vyanzo vya mapato .

Mgina, ametaja mkakati wa kufidia vyanzo hivyo kwa mwaka mpya wa Fedha 2016-2017 kuwa ni pamoja na kuanzisha stendi katika miji midogo ya Igowole na Nyololo, kuimarisha doria nyakati za usiku kwa wafanyabishara wanaotumia njia za panya kusafirisha mbao na Magogo hususani nyakati za usiku sanjari na kuongeza vizuio katika vijiji.
Share:

0 comments:

Post a Comment

Copyright © WAZO HURU | Powered by Blogger Design by ronangelo | Blogger Theme by NewBloggerThemes.com