METDO Tanzania

METDO Tanzania

Thursday, June 25, 2015

CAG aahidi kuing’arisha Tanzania kimataifa

Mkaguzina Mdhibiti mkuu wa hesabu za serikali (CAG), Profesa Mussa Assad

MDHIBITI na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), Profesa Mussa Assad ambaye pia ni mjumbe wa Bodi ya Ukaguzi ya Umoja wa Mataifa (UNBoA) amesema Tanzania itaendelea kuwa kinara katika shughuli za ukaguzi wa Umoja wa Mataifa ili kuweza kuiletea nchi sifa katika eneo la ukaguzi wa hesabu za umoja huo.


Aliyasema hayo wakati akizungumza na Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Ombeni Sefue wakati wa maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yaliyokuwa yakifanyika katika viwanja vya Mnazi Mmoja Dar es Salaam.

Alisema tangu Tanzania iteuliwe kujiunga na UNBoA mwaka 2012 na kuwasilisha taarifa yake ya kwanza ya ukaguzi kwa mwaka 2013, imefanikiwa kukagua na kuwasilisha jumla ya ripoti 14 za ukaguzi wa Mashirika ya Umoja wa Mataifa na kukubalika na Bodi ya Ukaguzi ya Umoja wa Mataifa.

“Tangu tujiunge na UNBoA mwaka 2012, tumefanikiwa kufanya kaguzi hizi na kutoa ripoti kwa wakati kwa miaka miwili mfululizo. Hivyo, ni ahadi yetu kwa Serikali na Watanzania wote kuwa hatutaiabisha serikali na nchi yetu,” alisema CAG.

Kwa mujibu wa Profesa Assad, Tanzania inatarajia kuwasilisha taarifa za ukaguzi za mashirika sita (6) mwezi ujao. Mashirika ambayo Tanzania inaendelea kufanya ukaguzi ni pamoja na Shirika la Mpango wa Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP).

Mengine ni Shirika la Idadi ya Watu Duniani la Umoja wa Mataifa (UNFPA), Shirika la Ujenzi na Misaada la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia Wakimbizi wa Palestina na Mashariki (UNRWA).

Upo pia Mfuko wa Akiba kwa Watumishi wa UNRWA Wakazi (UNRWA-SPF), Shirika la Usawa wa Jinsia na Uwezeshaji wa Wanawake (UN-Women) na Shirika la Ukuzaji Mitaji la Umoja wa Mataifa (UNCDF).

Assad alisema ripoti za mashirika tisa za ukaguzi wa Mashirika ya Umoja wa Mataifa zilizosalia zitatokana na ukaguzi unaofanywa na Ofisi za Ukaguzi za Hesabu za Serikali za China na Uingereza.

Alitumia fursa hiyo kuishukuru Serikali na Katibu Mkuu Kiongozi kwa ushirikiano mkubwa wanaoendelea kuipa Ofisi ya Taifa ya Ukaguzi hali inayoiongezea ufanisi Ofisi hiyo.

Share:

0 comments:

Post a Comment

Copyright © WAZO HURU | Powered by Blogger Design by ronangelo | Blogger Theme by NewBloggerThemes.com