METDO Tanzania

METDO Tanzania

Thursday, July 9, 2020

ALIYEKUWA RAS SIMIYU AMKABIDHI OFISI MRITHI WAKE

 Aliyekuwa Katibu Tawala wa Mkoa wa Simiyu, Bw. Jumanne Sagini (kushoto) akimkabidhi Katibu Tawala mpya wa Mkoa huo, Bi. Miriam Mmbaga nyaraka mbalimbali ikiwa ni ishara ya makabidhiano ya Ofisi yaliyofanyika mjini Bariadi 08 Julai, 2020.
Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony Mtaka (wa nne kushoto) akiwa na Katibu Tawala wa Mkoa wa Simiyu, Bi. Miriam Mmbaga (wa nne kulia) Mkuu wa Wilaya ya Maswa, Dkt. Seif Shekalaghe (kushoto), Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Maswa, Dkt. Fredrick Sagamiko (wa tatu kulia), Katibu wa itikadi na uenezi CCM Mkoa wa Simiyu, Bw. Mayunga George (wa pili kulia) na aliyekuwa Katibu Tawala wa Mkoa wa Simiyu, Bw. Jumanne Sagini (wa  tatu kushoto )na familia yake, wakiwa na zawadi ya unga waliopewa na Halmashauri ya Wilaya ya Maswa , ikiwa ni ishara ya kutambua mchango wa kiongozi huyo anayeondoka, mara baada ya makabidhiano ya Ofisi kati katibu Tawala wa Mkoa Mpya na anayeondoka, 08 Julai, 2020.
Aliyekuwa Katibu Tawala wa Mkoa wa Simiyu, Bw. Jumanne Sagini amemkabidhi rasmi ofisi mrithi wake Bi. Miriam Mmbaga ambaye aliteuliwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Magufuli Julai 03, 2020 kuchukua nafasi hiyo.

Makabidhiano hayo yamefanyika Julai 08, 2020 mjini Bariadi na kushuhudiwa na baadhi ya viongozi wa Chama na Serikali, viongozi wa dini, wakuu wa mashirika na taasisi za umma na binafsi pamoja na watumishi.

Akizungumza kabla ya makabidhiano hayo Sagini amemshukuru Mhe. Rais kwa kumuamini na kumteua ili aweze kuwatumikia wananchi kwa nafasi ya Katibu Tawala wa Mkoa huku akiwashukuru viongozi, watumishi na wananchi wa mkoa wa Simiyu kwa ushirikiano waliompatia katika kipindi chote alichokuwepo Simiyu.

“Namshukuru sana Mhe. Rais kwa imani yake kwangu nakumbuka mwezi Desemba 2015 alipoteua Makatibu Wakuu, makatibu wakuu tisa tuliachwa tukapangiwe kazi nyingine lakini baada ya muda akaniteua kuwa katibu tawala wa mkoa, nakumbuka katika wale tisa ni mimi peke yangu ndiyo niliteuliwa kuwa katibu tawala wa mkoa; hii ni imani kubwa sana kwangu,” alisema Sagini.

Aidha, Sagini ametoa wito kwa viongozi, watumishi na wananchi na wadau mbalimbali wa mkoa wa Simiyu kumpa ushirikiano Katibu Tawala mpya wa mkoa kama walivyokuwa wanampa yeye ili aweze kutimiza wajibu na majukumu yake kama inavyotakiwa.

Wakizungumzia aliyekuwa Katibu Tawala wa Mkoa wa Simiyu, Bw. Jumanne Sagini viongozi wa serikali, chama, wakuu wa taasisi na watumishi wamesema Sagini alikuwa kiongozi na mwalimu wao katika utendaji kazi wao huku wakibainisha kuwa amewasaidia katika utatuzi wa changamoto mbalimbali za kiutendaji.

“Sagini tumeshirikiana naye katika kipindi chote tulichokuwa pamoja naye, amefanya kazi iliyoacha alama kwenye mkoa hata zawadi alizopewa hapa ni moja ya alama za kazi yake nzuri, tunamtakia kila la heri; nitumie nafasi hii pia kumkaribisha RAS wetu mpya mimi na wenzangu tunakuhakikishia kukupa ushirikiano,” alisema Mhe. Anthony Mtaka Mkuu wa Mkoa wa Simiyu.

“Binafsi kaka yangu Sagini alikuwa si kiongozi tu bali mwalimu  kwangu amenifundisha vitu vingi sana maana mimi nimefanya kazi muda mfupi sana serikalini, miaka mingi nimefanya kazi katika sekta binafsi na nilikuwa sijui mambo mengi , yeye ndiye aliyenielekeza namna sahihi ya kutekeleza majukumu yangu,” alisema Mkuu wa wilaya ya Busega Mhe. Tano Mwera.

“Tunampongeza ndugu yetu Sagini kwa namna alivyokiunganisha Chama Cha Mapinduzi na watendaji wa Serikali kuanzia ngazi ya kijiji hadi mkoa mawasiliano na mahusiano kati yetu sasa hivi yameimarika sana; pia nampongeza  kwa namna alivyokuwa mwepesi kushughulikia changamoto za watumishi, wananchi na viongozi wa chama alizokuwa anapelekewa,” katibu wa itikadi na uenezi CCM Mkoa wa Simiyu, Bw. Mayunga George.

Kwa upande wake Katibu Tawala wa Mkoa wa Simiyu, Bi. Miriam Mmbaga amemshukuru Mhe. Rais kwa kumteua kushika nafasi hiyo huku akiahidi kushirikiana na wadau wote  kuendelea kuleta matokeo chanya katika mkoa ili uendelee kuwa mkoa bora ndani ya nchi na Afrika Mashariki na watu wengine wajifunze Simiyu.

Aidha, Bi. Mmbaga ametoa wito kwa watumishi kuzingatia nidhamu katika utumishi wao kwa kufuata sheria, kanuni na taratibu na kuwataka kila mmoja atimize wajibu wake huku akibainisha kuwa kila mtu akitimiza wajibu wake kero mbalimbali za wananchi zitatatuliwa na rasilimali za umma zitaokolewa. 
Bw. Jumanne Sagini alikuwa ni Katibu Tawala wa Mkoa wa pili tangu mkoa wa Simiyu uanzishwe mwaka 2012 na alikabidhiwa rasmi ofisi na mtangulizi wake Bi. Mwamvua Jilumbi Mei 02, 2016.
Share:

0 comments:

Post a Comment

Copyright © WAZO HURU | Powered by Blogger Design by ronangelo | Blogger Theme by NewBloggerThemes.com