
Na Eric Msuya – MAELEZO
Siku chache baada ya kutokea kwa
Uvumi wa kuwepo kwa Ugonjwa wa Ebola Nchini, Wizara ya Afya, Maendeleo
ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kupitia Waziri wake Mhe. Ummy Mwalimu
amewataka Wananchi wa Tanzania kutokuwa na hofu ya Ugonjwa huo kwani
hakuna dalili wala Mgonjwa aliyethibitishwa kuwa na ugonjwa wa Ebola.
Akizungumza na Waandishi wa Habari
jijini Dar es Salaam, Mhe. Ummy Mwalimu amewahakikishia Wananchi, kuwa
tangu kuripotiwa kwa Ugonjwa huo wa Ebola Nchi jirani, Serikali ya
Tanzania imeweka mikakati mbalimbali ya kulinda Afya za Watanzania.
“Tumeimarisha utaratibu na
ufuatiliaji wa Ugonjwa huu wa Ebola kupitia wataalamu wa Afya katika
Mikoa, Wilaya na kuimarisha Uchunguzi wa Wageni wanaoingia Nchini
kupitia mipaka yetu ya Tanzania” Alisema Mhe. Ummy Mwalimu
Sambamba na hilo Serikali kupitia
Wizara ya Afya imenunua Vipima Joto vya Mkono na Mavazi kinga (PPE)
seti 2,670 na kusambaza katika mikoa ya Kigoma, Kagera, Mwanza, Rukwa na
Katavi kutokana na kuwepo kwa hatari ya kukumbwa na Ugonjwa huo.
Wizara ya Afya inaendelea kuandaa
mpango mkakati wa kutengeneza Kitini na kutoa Elimu na Mafunzo ya
kukabiliana na Ugonjwa wa Ebola kupitia Waganga Wakuu wa Mikoa yote
nchini pamoja na Watumishi 724 wa sekta ya Afya na Ngazi ya Jamii.
“Tumeanda Kitini chenye maelezo
muhimu ya jinsi ya kukabiliana na Ugonjwa huu wa Ebola ikiwa sambamba na
kutoa Elimu kupitia Vyombo vya Habari kwenye vitu mbalimbali kama vile
Makala fupi zinazotolewa na Waandishi wa Habari kwa kuandaliwa na
Wizara ya Afya” Alisema Ummy Mwalimu
Aliongeza kuwa Wizara imetoa
Mafunzo juu ya kujikinga na Ugonjwa wa Ebola kwa Watumishi wa Afya zaidi
ya 460 na Ngazi ya Jamii zaidi ya 264, wakiwemo Viongozi wa Dini,
Wanahabari, Vijana wa Bodaboda pamoja na Watendaji wa Vijiji walio
katika Mikoa iliyo hatarini.
Serikali kupitia Wizara ya Afya
imejenga uwezo na kununua Vifaa Tiba katika Maabara Kuu ya Taifa Jijini
Dar es Salaam, Hospitali ya Rufaa ya Kanda ya Mbeya pamoja na Kituo cha
Utafiti wa Magonjwa wa Tiba (KCRI) kilichopo katika Hospitali ya KCMC
Mjini Moshi.
Waziri Ummy amewataka Wananchi
kutopuuzia Dalili zozote zitakazo tokea kwenye Miili yao kwa kufika
katika kituo cha Afya sababu Ugonjwa wa Ebola hauna tofauti na Dalili za
Homa na Maralia
“Dalili kuu za ugonjwa wa Ebola ni
Homa kali, kuumwa na kichwa, kutapika na kuharisha, viungo vya mwili
kuuma, kutokwa na Vipele Mwilini na Damu katika Matundu ya Mwili”
Alisema Ummy Mwalimu.
Wizara ya Afya imewataka Wanachi
katika Mikoa yote Tanzania kujikinga na kudhibiti Ugonjwa huu usiingie
Nchini kwa kuepuka kugusa Damu, Mkojo, Jasho, Kinyesi, kunawa Mikono
kupitia maji ya nayotiririka na kuepeuka Majimaji yanayotoka mwilini mwa
mgonjwa mwenye Dalili za Ebola.
“Lakini pia tuna namba za simu
Bure ambazo tumekuwa tukizisambaza kwa Wananchi ambazo ni 0800110124 au
0800110125 hivyo wananchi watoa taarifa endapo akiziona dalili za
ugonjwa wa Ebola” Alisema Ummy Mwalimu
Aidha, Waziri Ummy amewataka
Wananchi wasidanganyike na kuepuka kusikiliza Habari za Uvumi wa Ugonjwa
huo kutoka kwa Watu Mbalimbali wenyenia Ovu kwa Watanzania hivyo chombo
pekee chenye kuweza kutoa taarifa za Magonjwa ya milipuko ni Wizara ya
Afya.
“Kwa mujibu wa Sheria ya Afya ya
Jamii Na. 1 ya Mwaka 2009, dhamana ya kutoa Taarifa za Magonjwa ya
milipuko ukiwemo huu wa Ebola ni Wizara yenye dhamana na Masuala ya
Afya, hivyo kwa sasa hakuna Ugonjwa wa Ebola Nchini.” Alisisitiza Ummy
Mwalimu
0 comments:
Post a Comment