METDO Tanzania

METDO Tanzania

Saturday, March 10, 2018

"TANGU NIMCHAGUE DOTO BITEKO KUWA NAIBU WAZIRI ANAFANYA KAZI NZURI MNO" RAIS MAGUFULI


Na Mathias Canal, Runzewe-Geita

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt John Pombe Magufuli amewaambia wananchi Wilayani Bukombe Mkoani Geita kuwa wamepata Mbunge Doto Biteko ambaye ni mwaminifu kwao na serikali kwa ujumla hivyo wanapaswa kumuunga mkono ili atekeleze majukumu yake kwa ufasaha kwa mujibu wa ilani ya uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi ya mwaka 2015-2020.

Rais Magufuli ameyasema hayo wakati akihutubia mamia ya wananchi wa Wilaya ya Bukombe wakati wa uzinduzi wa barabara ya Uyovu-Bwanga yenye urefu wa kilomita 45 huku akisisitiza kuwa tangu amchague Mhe Biteko (Mb) kuwa Naibu Waziri wa Madini anafanya kazi nzuri kwa manufaa ya watanzania.

"Ndugu zangu wananchi mimi nitawashangaa sana kama mtaanza kubadilika badilika nakumbuka nilikuja hapa nikawaomba kura na nikamuombea kura Doto na nyinyi baada ya kumpa kura nyingi nikaamua kumpa unaibu Waziri ili awatumikie vizuri" Alikaririwa Mhe Rais Dkt Magufuli

Rais Magufulu alisema kuwa, Mhe Biteko alikuwa mwenyekiti wa kamati Maalumu ya Bunge ya kuchunguza uchimbaji na biashara ya Madini ya Tanzanite hivyo akafanya kazi nzuri ya kujitoa kwa ajili ya watanzania.

JPM kwa msisitizo mkubwa ameongeza kuwa wakazi wa Jimbo la Bukombe wana Mbunge mzuri ambaye anawasemea kila kitu hivyo uwepo wake serikalini utaongeza tija na manufaa kwa watanzania.

"Yaani waheshimiwa wananchi Hamkukosea kumchagua Mbunge Doto tena niwaambie sijui kama mtampata Doto mwingine inawezekana ana sura mbaya lakini ni kiongozi bora tena bado kijana anapaswa kuwatumikia vyema wananchi kwani ndio mtakaomsaidia katika maisha yake ya badaye" Alisisitiza Rais Magufuli

Pasina hiyana hapo hapo Rais Magufuli alimgeuzia kibao Mhe Doto na kumsihi kwa sifa hizo asije akabweteka kwani wananchi na Taifa kwa ujumla linamtegemea sana.

Naye Mbunge wa Jimbo hilo la Bukombe Mhe Doto Mashaka Biteko amempongeza Rais Magufuli kwa namna ya kipekee ya ufanyaji kazi kwani amewakumbuka wananchi wa Wilayani ya Bukombe ambapo pamoja na Ujenzi wa barabara aliyoizindua ya Uyovu-Bwanga yenye urefu wa kilomita 45 pia alitoa fedha kwa ajili ya Ujenzi wa shule ya msingi Ibamba, ambayo ipo kwenye Kata ya Uyovu kwani baada ya tangazo la elimu bure jumla ya wanafunzi 1250 walijiandikisha darasa la kwanza hivyo Rais Magufuli akaamua kuongeza Ujenzi wa vyumba vya madarasa 8 na matundu 20 ya vyoo ili kukabiliana na wingi wa wanafunzi hao.

Pia alimshukuru Rais Magufuli kwa kutenga fedha kwa ajili ya Ujenzi wa barabara ya kutoka Uyovu kuelekea Namonge mpaka Malandula, kutoa kiasi cha shilingi milioni 500 kwa ajili ya Upanuzi wa kituo cha afya Uyovu, jumla ya milioni 400 kwa ajili ya Ujenzi wa kituo cha afya cha Ushirombo na magari mawili kwa ajili ya kubeba wagonjwa (Ambulance).

MWISHO.
Share:

0 comments:

Post a Comment

Copyright © WAZO HURU | Powered by Blogger Design by ronangelo | Blogger Theme by NewBloggerThemes.com