METDO Tanzania

METDO Tanzania

Friday, June 26, 2015

Costech yapongezwa tafiti za ndani

Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, Profesa Makame Mbarawa

WAZIRI wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia Profesa Makame Mbarawa amesema Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia (Costech) imefanya kazi kubwa kuhamasisha matumizi ya sayansi na teknolojia nchini na sasa kuna taasisi ambazo zinatengeneza bidhaa ambazo zinasambazwa ndani na nje ya nchi.


Akizungumza kwenye kongamano la nne la Sayansi, Teknolojia na Ubunifu linaloendelea jijini Dar es Salaam, Profesa Mbarawa alisema chini ya usimamizi wa Costech kuna bidhaa zinazotokana na watafiti wa ndani ambazo zinauzwa katika nchi za Malawi na Zambia.

Waziri huyo pia alisema hadi sasa Costech imedhamini miradi 56 katika sekta ya kilimo, uvuvi kwa ajili ya kufanya tafiti mbalimbali ambazo alisema matokeo ya tafiti hizo yameleta matokeo mazuri na kuvutia wawekezaji wa nje kuja kujenga viwanda hapa nchini.

Alitoa mfano wa utafiti wa dawa ya kuchanja kuku dhidi ya ugonjwa wa mdondo ambao umefanywa na Chuo Kikuu cha Kilimo cha Sokoine chini ya uongozi wa Profesa Philemon Wambura kwamba utafiti huo umevutia wawekezaji kutoka Morocco.

Mfano mwingine ni utafiti uliofanywa na Taasisi ya Utafiti wa Magonjwa ya Binadamu (NIMR) juu ya kikombe cha babu wa Loliondo. “Utafiti huu ulibaini kuwa dawa ya babu haikuwa tiba ya ugonjwa wa kisukari na Ukimwi, lakini pia ile dawa haikuwa na madhara kwa binadamu,” alisema waziri huyo.

alisema utafiti mwingine ambao ulifanywa kwa mfumo huo ni ulinzi wa polisi jamii ambao umebaini kuwepo kwa idadi kubwa ya wananchi ambao wanatoa taarifa nyingi za uhalifu chini ya mpango huo.

Pia alisema utafiti mwingine ulihusu mradi wa uandishi wa kitabu cha Mwalimu Julius Nyerere maarufu kama wasifu wa Mwalimu Nyerere ambao kutokana na kitabu hicho Costech imeanzisha Kavazi la Mwalimu Nyerere.
Kavazi la Mwalimu Nyerere ni kituo huru kilichoanzishwa ndani ya Costech mwaka 2014. Majukumu yake ni kuhifadhi nyaraka zilizokusaywa na waandishi wa Bayografia ya Mwalimu Nyerere ili zitumiwe na watafiti.

Kutoa nafasi ya mijadala ya kizuoni na kimkakati juu ya masuala muhimu ya maendeleo ya jamii, kuandaa na kuendesha mafunzo ya nadharia na mbinu za utafiti wa masuala ya maendeleo ya jamii.

CREDIT: HABARI LEO

Share:

0 comments:

Post a Comment

Copyright © WAZO HURU | Powered by Blogger Design by ronangelo | Blogger Theme by NewBloggerThemes.com