Na Stella Kalinga, Simiyu
Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Mhe. Angelina Mabula(Mb),
ameziagiza Halmashauri nchini, kuyatambua na kuyatolea taarifa maeneo yanayohodhiwa na watu bila kuendelezwa
na yale ambayo hayakupatikana kihalali ili Wizara iweze kuchukua hatua stahiki.
Naibu Waziri huyo ameyasema hayo alipotembelea eneo la hekta 13 katika Kijiji
cha Kalago, Kata ya Lamadi, Wilayani Busega lililokuwa linamilikiwa na Mwekezaji
Hermati Pateli kinyume cha sheria, ambaye amefutiwa hati na Serikali, kisha
Halmashauri ya Busega Mkoani Simiyu kuanza ujenzi wa mradi wa maji katika eneo
hilo utakaonufaisha vijiji vinne vya kata ya Lamadi.
Mhe.Mabula amesema Halmashauri zinapaswa kutambua maeneo yasiyoendelezwa na
yanayomilikiwa kinyume cha sheria na kuwasilisha taarifa katika Wizara ya
Ardhi,Nyumba na Maendeleo ya Makazi ili yaweze kuyarejesha kwa wananchi na kupangiwa
matumizi mengine yenye manufaa zaidi kwa jamii.
“Maeneo yote yaliyohodhiwa ambayo hayajaendelezwa na ambayo pengine
hayakupatikana kihalali, ni jukumu la Halmashauri kuyatambua na kuleta taarifa zake Wizarani ili Wizara iweze
kuchukua hatua ya kuweza kuyarudisha katika matumizi kwa Umma na yaweze kufaidisha
watu wengi zaidi badala ya mtu mmoja” amesema Naibu Waziri Angelina Mabula
Aidha,Naibu Waziri Mabula amebainisha sababu
zilizopelekea Mwekezaji Hermati Pateli kufutiwa hati ya eneo hilo na Serikali kuwa ni udanganyifu
wa Uraia pamoja na upatikanaji wa hati ambao haukuzingatia sheria na taratibu za
nchi.
Naibu
Waziri huyo amesema eneo lililokuwa linamilikiwa na Mwekezaji huyo isivyo
halali ambalo limefutiwa hati miliki limegawanyika katika ploti mbili, ploti
Namba 01 na Namba 02 Block C lenye ukubwa
wa hekta 7.62 na Block Namba 03 C hekta 5.45.
Akitoa
maelezo kwa Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Mhe.
Angelina Mabula(Mb), Mhandisi Mshauri wa Mradi wa Maji wa Lamadi kutoka Kampuni
ya EAU Consult, Baraka Felix amesema Tanki la Maji litakalojengwa katika eneo
hilo litakuwa na uwezo wa kuzalisha mita za ujazo 3000 kwa siku.
Naye
Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Busega, Anderson Njiginya
amesema Mradi wa Maji wa Lamadi
unaojengwa katika eneo hilo utawanufaisha wananchi wa Vijiji Vinne vya Kalago,
Lamadi, Lukungu na Mwabayanda.
Mradi huu wa maji unaojengwa katika eneo hili
lililokuwa linamilikiwa isivyo halali na Mwekezaji Pateli, utagharimu kiasi cha
Yuro milioni 2.8, na unatarajiwa kukamilika ifikapo Mei, 2019.
Mhandisi Baraka Felix kutoka Kampuni ya EAU Consult akitoa maelezo kwa Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Mhe.Angelina Mabula(Mb)(kulia) alipotembelea kuona Ujenzi wa Ofisi ya Mamlaka ya Maji Lamadi itakayosimamia mradi wa maji wa Lamadi unaojengwa katika eneo lililokuwa linamilikiwa na Mwekezaji Hermati Pateli kinyume cha sheria, ambaye amefutiwa hati na Serikali .
Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Mhe.Angelina Mabula(Mb)(kushoto) akizungumza na waandishi wa habari katika mahojiano maalum mara baada ya kutembelea eneo la hekta 13 katika Kijiji cha Kalago, Kata ya Lamadi, Wilayani Busega lililokuwa linamilikiwa na Mwekezaji Hermati Pateli kinyume cha sheria, ambaye amefutiwa hati na Serikali.
Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Mhe.Angelina Mabula(Mb) (kushoto) akipokea maelezo kutoka kwa Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Busega, Anderson Njiginya wakati alipotembelea eneo la hekta 13 katika Kijiji cha Kalago, Kata ya Lamadi, Wilayani Busega lililokuwa linamilikiwa na Mwekezaji Hermati Pateli kinyume cha sheria, ambaye amefutiwa hati na Serikali.
Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Mhe.Angelina Mabula(Mb) (wa pili kushoto) akizungumza na baadhi ya Viongozi wa Wilaya ya Busega mara baada ya kutembelea eneo la hekta 13 katika Kijiji cha Kalago, Kata ya Lamadi, Wilayani Busega lililokuwa linamilikiwa na Mwekezaji Hermati Pateli kinyume cha sheria, ambaye amefutiwa hati na Serikali, (kushoto) Mkuu wa Wilaya hiyo, Mhe.Tano Mwera.
Msajili Msaidizi wa Baraza la Ardhi Kanda ya Ziwa, Dorothy Moses akitoa ufafanuzi juu ya hoja mbalimbali zilizowasilishwa na watumishi wa Idara ya Ardhi katika kikao cha Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi , Mhe.Angelina Mabula(Mb) na watumishi hao Wilayani Busega(hawapo pichani).
0 comments:
Post a Comment