METDO Tanzania

METDO Tanzania

Monday, August 28, 2017

DC MTATURU AMWAGA VIFAA VYA MICHEZO KWA TIMU 69 ZINAZOSHIRIKI MASHINDANO YA IKUNGI ELIMU CUP 2017


Mkuu wa Wilaya ya Ikungi mhe Miraji J. Mtaturu akifungua mipira aliyoigawa kwa timu zote shiriki za mashindano ya mpira wa miguu maarufu kama "IKUNGI ELIMU CUP 2017"

Mkuu wa Wilaya ya Ikungi mhe Miraji J. Mtaturu akionyesha moja ya mipira aliyoigawa kwa timu shiriki kwenye mashindano ya mpira wa miguu maarufu kama "IKUNGI ELIMU CUP 2017"
Baadhi za jezi zilizotolewa kwa ajili ya timu zote shiriki kwenye mashindano ya mpira wa miguu maarufu kama "IKUNGI ELIMU CUP 2017" 
Ugawaji wa vifaa vya michezo kwa timu shiriki kwenye mashindano ya mpira wa miguu maarufu kama "IKUNGI ELIMU CUP 2017"
Baadhi ya wananchi wakifatilia mechi ya ufunguzi wa mashindano ya mpira wa miguu maarufu kama "IKUNGI ELIMU CUP 2017" mara baada ya kufunguliwa na katibu tawala Mkoa wa Singida kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Singida
  
Na Mathias canal, Singida

Takribani timu 69 zinazoshiriki  mashindano ya mpira wa miguu maarufu kama “IKUNGI ELIMU CUP 2017” zimekabiziwa jezi pamoja na mipira kwa ajili ya utimilifu wa kuwa na vifaa vya michezo kwenye mashindano hayo jambo ambalo limeibua hisia chanya kwa kila timu kutaka kuibuka mshindi.

Akitoa vifaa hivyo vya michezo kwa ajili ya ushiriki wa timu hizo, Mkuu wa Wilaya ya Ikungi Mhe Miraji Jumanne Mtaturu alisema kuwa Ofisi yake kwa ushirikiano mkubwa na wadau wa elimu na wananchi kwa ujumla wamechangia vifaa hivyo vya michezo ikiwa ni sehemu ya kuongeza chachu ya hamasa katika mashindano na kufikisha zaidi ujumbe wa umuhimu wa waanchi kuchangia mfuko wa elimu.

Mashindano hayo yanayoshadihishwa na kauli mbiu isemayo CHANGIA, BORESHA ELIMU IKUNGI yanafanyika katika vijiji vyote 101 ambapo jumla ya Kata zote 28 zitashiriki na timu 69 zitapambana na kupatikana timu tatu bora.

Mhe Mtaturu alisema kuwa kunzishwa kwa mashindano hayo ni kusudio la kuifanya jamii kujihusisha na shughuli za maendeleo kwa kushirikiana na serikali, kuibua vipaji vya michezo katika Wilaya ili kukuza ajira na kufanya vijana waachane na utumiaji wa madawa ya kulevya.

Sababu zingine ni Kuunganisha jamii kuwa kitu kimoja hatimaye vijana na wananchi kuimarisha upendo, ajira na afya sambamba na kudumisha amani na mshikamano.

Mashindano hayo yanataraji kufika ukomo Septemba 19, 2017 huku zawadi zikitaraji kutolewa kwa washindi watano ambapo mshindi wa kwanza atapatiwa zawadi ya Kombe, Seti ya jezi, Mipira miwili na kitita cha shilingi 1,000,000/= , na mshindi wa pili atapatiwa Seti ya jezi, Mipira miwili na shilingi 750,000/=.

Mshindi wa tatu atapatiwa Mipira miwili na shilingi 450,000/= , Mshindi wa nne atapatiwa Mpira mmoja na Shilingi 200,000/= huku mshindi wa tano akipatiwa Mpira mmoja na Shilingi 100,000/=.

Aidha, kutakuwa na zawadi zingine kwa timu yenye nidhamu, Zawadi ya mfungaji bora, Zawadi ya Kipa bora, Zawadi ya mchezaji bora, huku wachezaji wengine 30 wakichaguliwa kuingia kambini kufundishwa mbinu za uchezaji bora.

Katika taarifa ya Mkuu wa Wilaya ya Ikungi Mhe Miraji Jumanne Mtaturu wakati wa uzinduzi wa ligi hiyo mbele ya Katibu Tawala wa Mkoa wa Singida Dkt Angelina M. Lutambi aliyemuwakilisha Mkuu wa Mkoa huo Mhe Dkt Rehema Nchimbi, alisema kuwa Idara ya elimu katika Wilaya hiyo inakabiliwa na changamoto mbalimbali ikiwemo upungufu wa nyumba za walimu, Upungufu wa Walimu, Maabara ya Masomo ya sayansi kwa shule za sekondari, pamoja na vifaa vya kujifunzia na kufundishia.

Hivyo Halmashauri ya Wilaya ya Ikungi kwa ushirikiano na Ofisi ya Mkuu wa Wilaya hiyo walianzisha mfuko wa elimu wilaya kwa mujibu wa sheria ndogo ya Halmashauri Wilaya ya Ikungi ya mwaka 2014 ambayo ilitolewa katika tangazo la serikali Na. 222 la tarehe 11 Julai, 2014 ili kuweza kukabiliana na changamoto za elimu ambazo zinaathiri mafanikio ya elimu katika Wilaya hiyo.

Kuanzishwa kwa mfuko wa elimu kumepelekea pia kufunguliwa kwa akaunti ya mfuko katika Benki ya NMB tawi la Ikungi kwa jina la Mfuko wa Elimu wa Wilaya ya Ikungi (Ikungi District Education Funds) akaunti Namba 52510000554.

Katika uzinduzi wa mashindano hayo pia ulizinduliwa mpango wa ufyatuaji tofali kila kata kupitia nguvu za wananchi ikiwemo kujitolea vifaa kama maji, Mashine Vibao na Mchanga kwa ajili ya ujenzi wa Maabara ya masomo ya Sayansi ambayo ipo katika hatua za msingi kwa muda mrefu.

Hata hivyo Mhe Mtaturu alitoa Rai kwa wadau wa elimu kuchangia mfuko wa elimu ili kukuza ufanisi wa elimu katika Wilaya hiyo ambao kwa kiasi kikubwa unategemea zaidi upatikanaji wa rasilimali fedha na nguvu kazi kutoka kwa wadau, wananchi, Taasisi, Mashirika, Makampuni mbalimbali yaliyopo ndani na nje ya nchi.

MWISHO
Share:

0 comments:

Post a Comment

Copyright © WAZO HURU | Powered by Blogger Design by ronangelo | Blogger Theme by NewBloggerThemes.com