Saturday, January 19, 2019

Waziri Biteko, Prof. Msanjila wautaka mgodi wa North Mara kutii mamlaka za Serikali


Katibu Mkuu wa madini, Prof. Simon Msanjila (kushoto) akieleza jambo katika kikao baina ya viongozi wa juu wa wizara na viongozi wa mgodi wa North Mara kilichofanyika tarehe 17 Januari, 2019 ofisini kwa Waziri wa Madini, Doto Biteko (kulia) jijini Dodoma.

Na Nuru Mwasampeta

Waziri wa Madini, Doto Biteko ameutaka uongozi wa mgodi wa North Mara kutii Mamlaka ya Serikali kwa kutekeleza maagizo yanayotolewa na mamlaka za Serikali nchini. 

Biteko alitoa kauli hiyo Jana tarehe 17 mwezi Januari katika kikao kilichoanza kwa utulivu mkubwa lakini kadri dakika zilivyokuwa zikisonga mbele kiligeuka kichungu na kuwapelekea wajumbe kutoka mgodi wa North Mara na Bulyanhulu kuridhia kuanza kuwalipa fidia wananchi wanaozunguka mgodi huo ambao wamekaa kwa muda mrefu pasipo kulipwa fidia zao.

Katika kikao hicho, Waziri wa Madini, Doto Biteko, alianza kwa kuwahoji viongozi wa mgodi wa North Mara na Bulyankulu juu ya  changamoto kubwa iliyopo katika eneo lao ambapo bila kusita walikiri wazi kuwa ni suala la malipo ya fidia ya ardhi kwa wananchi wanaouzunguka mgodi huo.

Akizungumzia ukiukwaji katika kutekeleza maagizo ya Serikali Waziri Biteko aliwaeleza wajumbe hao kuwa ili kuonesha wanatii mamlaka ya Serikali walipaswa kuwa wamechukua hatua kadhaa katika kuelekea kutatua changamoto hiyo.

Biteko alionesha kusikitishwa na mwitikio unaooneshwa na wawekezaji hao ambao kutoka kikao cha mwisho kilipokaa na kuafikiana kuanza kulipa fidia ya ardhi kwa wananchi wanaozunguka mgodi huo ni miezi minne na hakuna chochote kilichofanyika.

“Hatuwezi kuwa tunakaa, tunafikia maamuzi ninyi mnayapinga, ni nani yupo juu ya Serikali” Waziri Biteko alihoji. “Mnajua suala la ardhi ni kubwa sana, mnajua ni maelekezo ya Rais, sasa Rais ameagiza halafu hakitokei kitu! Mimi sielewi kabisa. Afadhali watu wangeanza kulipwa unaweza sema sasa hatua za malipo zinafanyika lakini kuko kimya”aling’aka.

Akizungumzia chanzo cha mgogoro kuchukua muda mrefu Biteko alisema ni tathmini iliyofanyika kwa mara ya pili  kupelekea kiasi cha fidia mgodi unaopaswa kuwalipa wananchi kuongezeka kutoka bilioni 1.6 hadi kufikia  bilioni 12.

Akifafanua hilo mara baada ya kuzungumza na mthaminishaji Mkuu wa Serikali (jina halikupatikana) kwa njia ya simu, Biteko alisema ameelezwa kwamba tathmini inayofuatwa ni ile iliyofanyika kwa mara ya pili maana hiyo ndiyo current na kukazia kuwa hawawezi kufuata ya awali kutokana na kwamba muda wa kuwalipa fidia hizo ulipaswa kutokuzidi miezi sita tangu tathmini kufanyika.

Ilielezwa kwamba, mara baada ya tathmini kufanywa kwa ajili ya malipo ya fidia, haipaswi kuzidi miezi sita na baada tu ya tathmini kufanyika; walipaswa kutoa tangazo ili kusimamisha uendelezaji wa maeneo ili kutokuongeza uwekezaji utakaopelekea wananchi kulipwa zaidi.

Biteko alieleza kuwa wananchi wanaomiliki maeneo hayo wakiendelea kufanya shughuli za maendeleo katika maeneo yao baada ya miezi sita kutoka tathmini ilipofanyika ni dhahiri kuwa gharama ya kumlipa fidia mwananchi huyo itaongezeka tu.

Aidha, Biteko aliwaeleza wajumbe hao kuwa uongozi wa mgodi huo hawazifuati mamlaka husika katika kutatua changamoto hiyo na kubainisha kuwa mgogoro huo hautatatuliwa na wizara ya Madini isipokuwa ni watu wenye mamlaka na masuala ya ardhi.

Akijibu hoja ya mmoja kati ya wajumbe kutoka North Mara aliyejaribu kueleza kuwa kiongozi mkuu wa masuala ya kisheria katika mgodi huo anayeishi nchini Uingereza ni sharti aelezwe pindi maamuzi na maagizo yeyote yanapopokelewa katika mgodi ili kufanya maamuzi yanayokidhi matakwa ya mgodi. Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini, Prof. Simon Msanjila alihoji endapo north Mara ipo juu ya Serikali?

Prof. Msanjila aliendelea kwa kusema haiwezekani mtu asiyekuwa na maamuzi katika mgodi kushiriki katika vikao vinavyojadili na kutoa maamuzi halafu mtu asiyeshiriki katika vikao hivyo akapinga maamuzi hayo.

“Yaani Waziri atoe maamuzi halafu mtu aliyeko Uingereza ayapinge that is totally subbodination maamuzi  ya mwisho yakishafanywa na Serikali hakuna serikali nyingine au kampuni yoyote ile iyapinge! Maamuzi yanayotolewa Tanzania hayawezi kwenda kujadiliwa London sio Sheria hiyo, ndio maana kampuni lazima iwe imesajiliwa Brella, kwa hiyo mambo ya kusema mshauri yupo London, South Africa No”. Alikazia Msanjila

“Don’t talk about London or South Africa tunapoongelea masuala ya Tanzania tunaongea  kwa sheria za Tanzania we have nothing to do with London hiyo ni yao” alisisitiza.

Msanjila aliwakumbusha makubaliano waliyoafikiana katika vikao vya nyuma kuwa yaliyowataka wajumbe wa vikao vya maamuzi wasiokuwa na nguvu ya kufanya nakutekeleza makubaliano ya kikao wasishiriki katika vikao hivyo ili kuepuka kupotezeana muda.

Huyu ni waziri, anamwakilisha Rais, hamuwezi kwenda kuomba ushauri London kwa maagizo yaliyotolewa na waziri, hiyo si sheria. Prof. Msanjila Alikazia.

Baada ya mahjiano makali na yaliyochukua muda mrefu kikao kilifikia muafaka na ujumbe kutoka North Mara kukiri kuwa kutokana ukweli kwamba baadhi ya wananchi waliofanyiwa tathmini malipo yao hayana shida watakwenda na kuanza kufanya taratibu za malipo.

Walikiri kuwa mara baada ya kufika katika vituo vyao vya kazi watakwenda kuendelea na taratibu za malipo ili kuonesha uungwana na kuionesha Serikali na jamii kuwa wamechukua hatua kwa makubaliano yaliyoafikiwa na viongozi wakuu wa nchi.

Aidha, walikiri kuwa wamejifunza kitu kutokana na kikao hicho na kukiri wanaendelea kujifunza kwani wameona madhara makubwa katika kuchelewesha malipo hayo na kuipelekea kampuni hasara kwa kulipa zaidi ya mara mbile ya kile walichotakiwa kulipa awali.

Zaidi ya hapo, wamejifunza juu ya uhalisia wa kisheria upande wa  tathmini ya ardhi kuwa huwa  hai kwa kipindi cha miezi sita na ikizidi hapo inafanyika tathmini nyingine lakini pia wamejifunza juu ya taratibu na sheria za kusitisha shughuli za maendeleo kwa wananchi kwa kutangaza kusimamisha shughuli za maendeleo katika maeneo yaliyofanyiwa tathmini kwa kipindi cha miezi sita na pia kulipa fidia kwa wakati ili wananchi wakajiendeleze katika maeneo mengine watakayohamia.

Aidha, Bi Jane Reuben- Lekashingo alisema kuwa si lengo lao kupinga maamuzi ya serikali ila wanachelewa kutokana na taratibu za kiutendaji wanaazopaswa kuzifuata  ili kukidhi matakwa na taratibu  za kampuni katika kutekeleza majukumu yao na kukiri kuwa sasa watasimamia sheria za nchi na kutekeleza makubaliano yaliyofikiwa katika vikao vya maamuzi.

No comments:

Post a Comment