Wednesday, November 21, 2018

Vituo vya Umahiri kuchochea shughuli za uongezaji thamani madini nchini- Kairuki


Waziri wa Madini Angellah Kairuki sambamba na Naibu Waziri Doto Biteko katikati mbele) wakikagua maendeleo  ya ujenzi wa kituo cha Umahiri cha Musoma


Waziri wa Madini Angellah Kairuki akiangalia ubora wa nondo zinazotumika katika ujenzi wa Kituo cha Umahiri.

Ø Asema baada ya Lwamgasa kituo kingine cha mfano kujengwa

Imeelezwa kuwa, vituo vya Umahiri vinavyojegwa maeneo mbalimbali nchini vinatarajiwa kuwa kichocheo cha shughuli za uongezaji thamani madini nchini kwa kuwa, vinatarajia kutoa mafunzo ya uchimbaji bora wa madini ikiwemo uongezaji thamani madini, ukataji na ung’arishaji madini.

Hayo yamebainishwa Novemba 20 na Waziri wa Madini Angellah Kairuki wakati alipofanya ziara ya kukagua maendeleo ya ujenzi wa kituo cha Umahiri cha Musoma kinachojengwa na Mkandarasi kampuni ya SUMAJKT na kusimamiwa na kampuni ya Sky Architects.

Katika ziara hiyo, Waziri Kairuki ameambatana na Naibu  Waziri wa Madini Doto Biteko, Mkurugenzi wa Sera na Mipango Augustine Ollal, Meneja wa Mradi wa Usimamizi Endelevu wa Rasilimali Madini, Andrew Eriyo pamoja na Watendaji wa  Ofisi ya Madini Mkoa wa Mara na uongozi wa Mkoa wa Mara.

Waziri Kairuki ameeleza kwamba, serikali imedhamiria kuhakikisha kuwa shughuli za uongezaji thamani madini zinafanyika nchini badala ya kusafirisha madini yakiwa ghafi na kuongeza kuwa,  uwepo wa vituo husika utaongeza shughuli  hizo kufanyika nchini kwa kuwa vitatoa elimu  ambayo itawezesha wachimbaji kufanya uchimbaji wenye tija.

Pia, amesema serikali itaendelea kuhamasisha shughuli za uongezaji thamani madini kufanyika nchini ikiwemo kuhakikisha kwamba inajenga  maeneo mengi zaidi ya vituo hivyo.

Vilevile, amezungumzia kituo cha mfano cha Lwamgasa kinachojengwa mkoani Geita, na kueleza kuwa, serikali inaangalia uwezekano wa kuwa na kituo kama hicho katika maeneo mengine na kuongeza, “tunaangalia sehemu nyingine baada ya kuwa na kituo cha mfano cha Lwamgasa huenda tukajenga kituo kama hicho hapa Musoma”.

Kituo cha Lwamgasa ni moja ya vituo ambavyo vinalenga katika kutoa mafunzo kwa  vitendo kwa wachimbaji wadogo wa madini ya dhahabu kuhusu uchimbaji wenye tija ikiwemo uchenjuaji bora pasipo kutumikia kemikali.

Kwa mujibu wa taarifa ya wizara ya tarehe 29 Oktoba,  kwa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini, wizara ilieleza kuwa kazi ya ujenzi wa mgodi wa Lwamgasa na usimikaji mitambo ya uchenjuaji katika kituo  hicho imekamilika kwa asilimia 80.

Akiwa kituoni hapo, Waziri Kairuki ameendelea kusisitiza kuhusu kuzingatia muda wa kukamilisha ujenzi huo ikiwemo kuzingatia ubora na viwango vya ujenzi vinavyotakiwa.

Pia, ameupongeza uongozi wa Mkoa kwa ushirikiano inaoonesha katika kufuatilia ujenzi huo na kuutaka kuendelea kushirikiana na wizara ili kuhakikisha kwamba azma ya kituo hicho inafikiwa.

Kwa upande wake, Afisa Madini Mkoa wa Mara, Mgaya Nyaisara  amesema kuwa, kituo kitatoa mafunzo ya namna ya uandaa sampuli za madini, namna ya kusafisha madini pia kutakuwa na mashine za kupima madini ya aina mbalimbali.

Naye w Mkandarasi SUMAJKT, katika taarifa iliyosomwa na Meja Onesmo Njau, amesema kuwa, kampuni hiyo itahakikisha inakamilisha ujenzi wa kituo hicho katika muda uliopangwa kimkataba na kueleza kuwa, ujenzi wa kituo hicho unaogharimu shilingi bilioni 1.2 ikijumuisha jengo la ofisi ya madini na kituo cha umahiri umefikia asilimia 35.

Vituo vya umahiri vinajengwa kupitia Mradi wa Usimamizi Endelevu wa Rasilimali Madini (SMMRP) kwa Benki wa Dunia

No comments:

Post a Comment