Saturday, September 8, 2018

NCHI ZA AFRIKA ZASISITIZA ULAZIMA WA KULETA MAGEUZI KATIKA SEKTA YA KILIMO, DKT TIZEBA ATAJA MKAKATI WA KUPUNGUZA UPOTEVU WA CHAKULA NCHINI TANZANIA

 Rais Paul Kagame wa Rwanda
Mhe Dkt Charles Tizeba, Waziri wa kilimo Tanzania
Na Mathias Canal, Kigali-Rwanda
Viongozi wa nchi za Afrika waliokutana katika mji mkuu wa Rwanda, Mjini Kigali wamekubaliana kuboresha hali ya sekta ya kilimo na kuongeza kiwango cha usalama wa chakula barani humo ikiwemo kupambana na kadhia ya upotevu wa chakula jambo ambalo bado ni changamoto kubwa inayohitaji kupatiwa ufumbuzi wa haraka.
Viongozi hao wamefikia makubaliano hayo katika kongamano la saba la Jukwaa la Mapinduzi ya Kijani ya kilimo na usalama wa chakula ambalo lilianza siku ya Jumatano ya tarehe 5 mwezi huu wa Septemba 2018 mjini Kigali.
Rais Paul Kagame wa Rwanda akihutubia washiriki wakati Wa kufunga kongamano la Mapinduzi ya kijani Barani Afrika (AGRF) lililofanyika Mjini Kigali likiongozwa na kauli mbiu isemayo "Ongoza, Pima, Kua: Kuwezesha njia mpya za kubadilisha wakulima wadogo kufanya kilimo biashara endelevu" amesema kuna ulazima wa kufanyika mageuzi na harakati katika sekta ya kilimo kwa ajili ya kuboresha hali ya kiuchumi na kijamii ya bara la Afrika.

Amefafanua kuwa kuinua kiwango cha uzalishaji katika sekta ya kilimo, mbali na kuongeza usalama wa chakula kutapunguza pia kiwango cha ukosefu wa ajira kwa vijana na akina mama wa Kiafrika.
Rais Paul Kagame wa Rwanda ametilia mkazo sekta binafsi kuongeza kiwango cha uwekezaji na kueleza kuwa kutengwa bajeti kwa ajili ya kuboresha ubora wa mbegu na kuimarisha sekta ya kilimo kutaleta ustawi kwa maisha ya Waafrika.
Washiriki wa kongamano la Jukwaa la Mapinduzi ya Kijani wameahidi pia kuchukua hatua za kisiasa na kiuchumi zinazohitajika ikiwemo kudhamini bajeti kwa ajili ya utumiaji teknolojia ya kisasa kwa lengo la kuleta mageuzi ya dhati katika sekta ya kilimo na chakula na hatimaye kufanikisha Mapinduzi ya Kijani barani Afrika
Jukwaa la Mapinduzi ya Kijani (AGRF) limeandaa kongamano kwa viongozi wa Afrika  na kuendesha mpangilio wa kukuza uwekezaji na sera ya kuongeza uzalishaji wa kilimo na ukuaji wa kipato kwa wakulima wa Afrika.
Watu zaidi ya 2000 wakiwemo wataalamu wa kilimo, viongozi wa serikali na maafisa waandamizi kutoka nchi 40 walioshiriki katika mkutano huo wa siku tano wameahidi kutumia fursa hiyo na kutoa dola milioni kadhaa za kimarekani katika uwekezaji mpya kwa wakulima wa Afrika na biashara zinazohusiana na kilimo.

Waziri wa kilimo nchini Tanzania Mhe Dkt Charles Tizeba (Mb) amesema mageuzi mapya yanahitajika katika sekta ya kilimo ili kuhimiza Afrika kuondokana na umaskini uliokithiri na kiwango cha chini cha uwekezaji.

Dkt Tizeba amesisitiza kuwa nchi ya Tanzania, kama zilivyo nchi zingine za Afrika, husumbuliwa na matatizo makubwa kadhaa ya uhifadhi chakula ambayo hupelekea upotevu wa rasilimali uzalishaji kama hazitashughulikiwa ipasavyo.

Aliyataja matatizo hayo kuwa ni pamoja na Teknolojia duni, hasa katika uvunaji na uhifadhi wa chakula baada ya mavuno, Ujuzi hafifu wa mnyororo wa matukio baada ya uvunaji, na Uhaba wa masoko na miundimbinu mibovu, kwani wazalishaji na wanunuzi hawana mawasiliano mazuri kutokana na uhaba wa taarifa na barabara zisizopitika katika misimu yote.

Aidha, matatizo mengine ni pamoja na Uhaba wa fedha katika shughuli mbalimbali baada ya uvunaji, Ushiriki hafifu wa sekta binafsi katika kuwekeza katika mchakato wa shughuli mbalimbali baada ya uvunaji, na katika hatua ya uhifadhi, upotevu hutokana na magonjwa na wadudu ambao husababisha upotevu katika ubora na kiasi.

Aliongeza kuwa upotevu wa chakula baada ya uvunaji umeendelea kuwa tatizo kubwa siyo tu katika chakula lakini pia katika malighafi kwa maendeleo ya viwanda huku akizitaja juhudi zilizofanywa na serekali ya Tanzania kupunguza upotevu wa chakula ambazo ni pamoja na kushirikiana na wadau mbalimbali wa maendelea, taasisi za kimataifa kama vile Bill and Melinda Gates foundation, HELVETAS Swiss Inter Cooperation Agency, Rockefeller foundation, AGRA, shirika la chakula duniani, mashirika yasiyo ya kiserikali ambayo yameboresha kwa kiasi kikubwa teknolojia ya uhifadhi kama vile mifuko ya plastiki ya kuhifadhia nafaka ambayo imeonesha kuwa na mafanikio makubwa sana kwa kuzuia wadudu waharibifu kupenya na kushambulia nafaka. 

Pia Kuanzishwa kwa mfumo wa ubadilishanaji bidhaa Tanzania. Kuweka mazao katika masoko yaonekanayo ili kurahisisha uuzaji na kupunguza upoteaji wa bidhaa za kilimo. Chini ya mradi huu mazao yatatunzwa chini ya mfumo vikundi vya wakulima na kuuzwa moja kwa moja  katika mfumo wa kubadilishana mazao.

Kongamano hilo limefikia ukomo hapo jana tarehe 8 Septemba 2018 baada ya kujadili maswala ya kilimo kwa siku nne mfululizo lilihudhuriwa pia na viongozi wengine wa Afrika akiwemo Rais wa Ghana Mhe Nana Addo Dankwa Akufo Addo, Makamu wa Rais wa Kenya Mhe William Ruto, Waziri Mkuu wa Gabon Mhe Emmanuel Issoze-Ngondet sambamba na Waziri Mkuu mstaafu wa Uingereza Mhe Tony Blair.

MWISHO.

No comments:

Post a Comment