SERIKALI KUWEKA BAYANA MAJINA YA WAKANDARASI WABABAISHAJI
Naibu Waziri wa Maji, Mhe. Jumaa Aweso
akiwa na Mhandisi wa Maji, Evaristo Mgaya kwenye eneo linapojengwa tenki
la maji la Mradi wa Maji wa Itigi katika Halmashauri ya Itigi, Wilaya
ya Manyoni, mkoani Singida.
Naibu Waziri wa Maji, Mhe. Jumaa Aweso
akiongea kwa simu na Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Nangai
Engineering Ltd alipokuwa akikagua Mradi wa Maji wa Itigi, uliopo katika
Halmashauri ya Itigi, wilayani Manyoni, mkoani Singida.
Naibu Waziri wa Maji, Mhe. Jumaa Aweso
akimsikiliza Mhandisi wa Maji Halmashauri ya Itigi, Evaristo Mgaya
kwenye moja ya vituo vya maji vinavyojengwa wakati akikagua Mradi wa
Maji wa Itigi, uliopo katika Halmashauri ya Itigi, wilayani Manyoni,
mkoani Singida. Kulia ni Mkuu wa Wilaya ya Itigi, Rahabu Mwangisa.
Naibu Waziri wa Maji, Mhe. Jumaa Aweso
akiwa kwenye kisima cha maji kilichopo eneo la Kanisani, moja ya visima 5
vya Mradi wa Maji wa Itigi, uliopo katika Halmashauri ya Itigi,
wilayani Manyoni, mkoani Singida.
………………
Serikali imesema itaweka bayana majina ya
makandarasi wote wanaoharibu miradi ya maji kwa kuitekeleza chini ya
kiwango na kuwachukulia hatua kali za kisheria katika hatua ya kumaliza
tatizo la utendaji mbovu kwenye kazi za miradi ya maji linalochangia
wananchi kukosa huduma ya maji.
Naibu Waziri wa Maji, Jumaa Aweso ametoa
kauli hiyo mara baada ya kutoridhishwa na Mkandarasi wa Kampuni ya
Nangai Engineering Ltd kufanya kazi kwa asilimia 30 ukilinganisha na
kiasi cha Shilingi milioni 250 alizolipwa, wakati mkandarasi wa Kampuni
ya Nipo Africa Ltd akiwa amefanya kazi kwa asilimia 68 huku akidai
fedha za malipo za ujenzi wa Mradi wa Maji wa Itigi uliopo katika
Halmashauri ya Itigi, Wilaya ya Manyoni, mkoani Singida alipokuwa
akikagua mradi huo.
‘‘Wakandarasi wababaishaji wa namna hii
wote tutawaanika hadharani na watachukuliwa hatua kali za kisheria na
Bodi ya Wakandarasi (CRB), Wakala wa Maji Vijijini (RUWASA) utakapoanza
Julai Mosi, 2019 utakuwa ni mwisho wa wakandarasi wababaishaji kupata
kazi za miradi ya maji ’’, amesema Aweso.
‘‘Serikali imelenga kufikisha huduma ya
maji kwa wananchi, hatutakubali mkandarasi au mtu yeyote kukwamisha
juhudi zetu za dhati za kumaliza tatizo la maji. Kuanzia sasa
tutaorodhesa wakandarasi wote wasio na sifa na kuwafungia wasipewe kazi
miradi yoyote ya maji nchini, ameelekeza Naibu Waziri.
Aidha, Aweso ameipongeza Kampuni ya Nipo
Africa Ltd kwa kufanya kazi nzuri, akiahidi kuyafanyia kazi madeni yao
na kuwalipa haraka. Pia, amewataka Wakurugenzi Watendaji wa Kampuni za
Nangai Engineering Ltd na Nipo Africa Ltd kukutana nae siku ya Alhamisi
Julai 20, 2019 kwenye kikao kitakaochuhusisha viongozi na wataalam wa
Sekta ya Maji mkoani Singida kitakacholenga kukwamua mradi huo uweze
kukamilika kwa wakati.
Wakati huo, Mkuu wa Wilaya ya Manyoni,
Rahabu Mwangisa amemshukuru Naibu Waziri kwa ahadi yake ya kumlipa
mkandarasi huyo na kumuahidi kuwa viongozi wa Wilaya ya Manyoni
watasimamia mradi huo kwa ukaribu uweze kukamilika haraka.
Ujenzi wa Mradi wa Maji Itigi umeanza
kutekelezwa mnamo 3/12/2018 na unategemewa kukamilika 2/9/2019 kwa zaidi
ya Shilingi bilioni 2.6 ukihusisha uchimbaji wa visima 5 virefu vyenye
uwezo wa kutoa jumla lita za ujazo 112,000 kwa saa, pamoja na ujenzi wa
miundombinu ya maji.
Mradi huu utakapokamilika unatarajiwa
kuhudumia vijiji 6 vya Songambele, Mlowa, Majengo, Tambukareli,
Zinginali na Itigi unahusisha Mradi wa Maji wa Itigi utakaogharimu
zaidi ya Shilingi bilioni 2.6.
No comments:
Post a Comment