Tuesday, June 18, 2019

Mhandisi Mtigumwe ajionea maandalizi ya Nane nane ambayo Kitaifa yatafanyika Mkoani Simiyu

Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo Mhandisi Mathew Mtigumwe akipata maelezo kuhusu kilimo shadidi kutoka kwa mtaalamu wa Kilimo Dkt Kisa Kajigili
Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo Mhandisi Mathew Mtigumwe akizungumza na Mkuu wa Mkoa wa Simiyu Mhe Antony Mtaka mara baada ya kuwasili Mkoani humo kujionea hmaandalizi ya maonesho ya Nanenane.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo Mhandisi Mathew Mtigumwe akiongozana na mtaalamu kutoka wizara ya Kilimo Dkt Kisa Kajigili wakati wa ukaguzi wa maandalizi ya maonesho ya Nanenane.

Na Mathias Canal, Wizara ya Kilimo - Simiyu

Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo Mhandisi Mathew Mtigumwe jana Tarehe 17 Juni 2019 alitembelea Viwanja vya Nyakabindi vilivyopo Mkoani Simiyu kujionea maandalizi ya maonesho ya Wakulima (Nanenane) ambayo hufanyika kila mwaka kuanzia Agosti 1-8 katika maeneo mbalimbali nchini.

Akiwa katika viwanja vya Nyakabindi Katibu Mkuu huyo alijionea maeneo mbalimbali likiwemo eneo la Wizara ya Kilimo na kujionea vipando vya mazao mbalimbali ambavyo vimefikia hatua nzuri.

Akizungumza na maafisa wa wa Wizara ya Kilimo sambamba na maafisa wa Mkoa wa Simiyu Mhandisi Mtigumwe alisisitiza kuwa wataalamu hao wanapaswa kuandaa vipando vya mazao  yote yenye tija kubwa ikiwemo Matunda na mboga mboga.

Kadhalika alisisitiza kuongezwa kasi ya maandalizi ambapo alitumia nafasi hiyo kuwaagiza Maafisa hao kufanya maandalizi mazuri yatakayokuwa Mfano kwa wadau wengine.

Aidha, baada ya kutembelea viwanja hivyo Mhandisi Mtigumwe alikutana na mwenyeji wake ambaye ni Mkuu wa Mkoa wa Simiyu Mhe Antony Mtaka ambapo walifanya mazungumzo kuhusiana na shughuli za Kilimo katika mkoa wa Simiyu.

Baada ya Ziara hiyo katika mikoa ya Shinyanga, Mwanza, Geita na Simiyu Mhandisi Mtigumwe amerejea Jijini Dodoma kuendelea na shughuli zingine.

MWISHO

No comments:

Post a Comment