Saturday, June 15, 2019

KATIBU MKUU CHAMA CHA FLERIMO CHA MSUMBIJI AWASILI JIJINI DODOMA

Na.Alex Mathias,Dodoma

KATIBU Mkuu wa Chama Cha Flerimo cha nchini Msumbiji Samwel Regue amewasili jijini Dodoma na kulakiwa na mgeni wake Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi(CCM)dokta Bashiru Ally.

Akiwa jijini humo pamoja na mambo mengine atafanya mazungumzo na Makamu Mwenyekiti wa CCM Bara mzee Philip Mangula kabla ya kuelekea wilayani Kibaha mkoani Pwani kuangalia maendeleo ya ujenzi wa Chuo Cha Uongozi.

Regue mara baada ya kuwasili katika uwanja wa ndege wa Dodoma pamoja na wenyeji wake walielekea ofisi za CCM Makao Makuu alipoandaliwa mapokezi na hapo alivishwa mavazi rasmi ya kabila ya wagogo ikiwa ni namna ya kukaribishwa.

Akizungumza katika mapokezi hayo dokta Bashiru amemshukuru Regue kwa ujio wake na kusema kuwa pamoja na kwenda Kibaha ataenda Zanzibar kwa ajili ya kuonana na raia wa Msumbiji wanaoishi huko.

“Mgeni wetu amewasili hapa,tumempokea na kwa mujibu wa ratiba atapata nafasi kutembelea ujenzi wa Chuo chetu pale Kibaha ambao unaendelea vizuri,

“CCM,Frelimo,ANC cha Afrika ya Kusini,NPLA cha Angola,SWAPO cha Namibia,ZANU PF cha Zimbabwe ni vyama ambavyo vimeungana kujenga chuo hicho kwa kushirikiana na chama cha Kikomunist cha nchini China”alisema dokta Bashiru.

No comments:

Post a Comment