Wednesday, February 13, 2019

MAKAMU WA RAIS AZUNGUMZA NA WASANII KWENYE KONGAMANO LA WASANII TANZANIA KUHUSU ATHARI ZA MATUMIZI NA BIASHARA YA DAWA ZA KULEVYA


Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akihutubia wasanii wa fani mbali mbali waliohudhuria  Kongamano Kuhusu Tatizo la Dawa za Kulevya kwa Wasanii lililoandaliwa na Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya pamoja na Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo leo februari 13, 2019 lililofanyika katika  Kituo cha Kimataifa cha Mwalimu Julius Nyerere, jijini Dar es Salaam. (Picha na Ofisi ya Makamu wa Rais)

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akiangalia kwa umakini Sanaa ya maigizo iliyokuwa ikionyeshwa na wasanii kutoka Taasisi ya Sanaa na Utamaduni Bagamoyo (TASUBA) waliokuwa wakionyesha madhara ya dawa ya kulevya wakati wa Kongamano Kuhusu Tatizo la Dawa za Kulevya kwa Wasanii lililoandaliwa na Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya pamoja na Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo leo februari 13, 2019 .Kongamano hilo limefanyika katika  Kituo cha Kimataifa cha Mwalimu Julius Nyerere, jijini Dar es Salaam. (Picha na Ofisi ya Makamu wa Rais)

Heshima kwa Godzilla; Wasanii wa Filamu na Muziki wakiwa wamesimama kwa dakika moja kama ishara ya kumkumbuka msanii wa hiphop Tanzania Golden Jacob Mbunda aliyefariki asubuhi ya leo kabla ya kuanza kuhutubia  Kongamano Kuhusu Tatizo la Dawa za Kulevya kwa Wasanii lililoandaliwa na Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya pamoja na Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo leo februari 13, 2019 lililofanyika katika  Kituo cha Kimataifa cha Mwalimu Julius Nyerere, jijini Dar es Salaam. (Picha na Ofisi ya Makamu wa Rais)

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan amewataka wasanii chini kuiga mambo yenye kuleta manufaa kwa jamii.

Makamu wa Rais ameyasema hayo leo jijini Dar es Salaam wakati akihutubia Wasanii wa Sanaa mbalimbali waliohudhuria Kongamano la Wasanii nchini dhidi ya tatizo la dawa za kulevya.

“Naamini kuwa wasanii hawa ni vioo vya jamii lakini baadhi yao wamekuwa wakitumika kama ‘mapunda’ kusafirisha dawa na wengine kudumbukia kwenye uraibu wa dawa za kulevya” alisema Makamu wa Rais.

Makamu wa Rais aliwaasa wasanii hao kujiepusha na matumizi na biashara ya dawa za kulevya ambapo aliwaambia dawa za kulevya zina madhara mengi kiuchumi, kisiasa, mazingira, kiafya na kijamii, pia hudhoofisha afya za watumiaji na kuathiri uwezo wa kufanya kazi.

Kongamano hilo lililobeba kauli mbiu inayosema Usanii bila kutumia au kubeba Dawa za Kulevya inawezekana, Chukua Hatua.

Makamu wa Rais amepongeza kwa kuanzisha vituo 6 vya huduma ya methadone ambapo jumla ya waathirika 6,300 wametibiwa kwenye vituo hivi.

Makamu wa Rais ameagiza Mamlaka ya Chakula na Dawa (TFDA) kuharakisha  miongozo hiyo na itakuwa vyema ikiwa kwenye udhibiti wa Dawa za hospitali zenye asili ya kulevya ili zitolewe na Bohari ya Kuu ya Madawa (MSD) badala ya watu binafsi.

Pamoja na mambo mengine Makamu wa Rais ametoa rai kwa vyombo vya ulinzi na usalama hususani polisi na maafisa uhamiaji kuhakikisha kuwa bidhaa zinazovuka mipaka yetu zisiwe bidhaa zinazokuja kuharibu Taifa.

Kwa upande mwingine Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Kazi, Vijana , Ajira na Walemavu) Mhe. Jenista Mhagama  alisema Serikali ya Awamu ya Tano chini ya Uongozi wa Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli amedhamiria kutokomeza dawa za kulevya hapa nchini.

Wakati huohuo, Waziri wa Habari, Utamaduni Sanaa na Michezo Mhe. Harisson George Mwakyembe alisema amefurahishwa na nia njema iliyoonyeshwa na wasanii ya vita dhidi ya matumizi na biashara ya dawa za kulevya. 

No comments:

Post a Comment