Monday, October 22, 2018

TGNP yawapika wana GDSS kuhusu swala la Uwajibikaji

Viongozi na wanajamii kutoka sehemu mbalimbali za jiji la Dar es salaam wahimizwa kuhusu maswala mtambuka ya kufahamu haki na wajibu wao katika uwajibikaji kwa ngazi ya mtaa na kata.
 Afisa Programu ya Harakati na Ujenzi wa Nguvu za Pamoja Anna Sangai akitoa ufafanuzi wa jambo fulani mbele ya washiriki wa semina.

Hayo yamesemwa mapema jana jijini Dar es salaam na Afisa Program ya Harakati na Ujenzi wa Nguvu za Pamoja wa TGNP, Dada Anna Sangai wakati akifungua mafunzo rasmi kwa ajili ya kuwajengea uwezo washiriki wa semina za GDSS kuweza kutambua haki na wajibu wao katika serikali zao za mitaa.

Katika semina hiyo iliyofanyika leo tarehe 20/10/2018 yenye lengo la kuwakutanisha wananchi wa jiji la Dar es salaam na kuweza kushirikishana mbinu mbalimbali, changamoto pamoja na kujenga mikakati ya uwajibikaji wa jamii katika ngazi ya mitaa pamoja na kata.

Afisa huyo amesema kuwa kama inawezekana mpango huo ungewekwa katika sharia ya nchi ili kuwataka wanasiasa kutotumia kigezo cha huduma za kijamii kama Maji, Umeme, huduma za afya pamoja na kuwapa wananchi vitenge, na kofia ili wawapigie kura na wakati huduma hizo ni haki yao ya msingi hata wasipopiga kura.
Washiriki wakifuatilia semina kwa umakini.

Aliendelea kusisitiza kuwa katika vuguvugu la ujenzi wa nguvu za pamoja ni vema washiriki kushirikishana uwezo na wenzao katika maeneo yao wanayoishi ili elimu walioipata iweze kusambaa kwa sehemu kubwa zaidi katika jamii.

Kwa upande wake Muwezeshaji wa semina hiyo Ndugu Geofrey Chambua amesema kuwa bado kuna changamoto kubwa kwa upande wa uwajibikaji katika serikali zetu za mitaa kwa kuwa wananchi wengi wanakosa ushirikiano kutoka kwa baadhi viongozi wao.

Aliendelea kusisitiza kuwa hii inatokana na viongozi wengi wanajiona wao wapo juu ya wananchi hali inayofanya kufanya mambo kwa namna wanavyojisikia nakujisahau kuwa wapo kwa ajili ya kuwatumikia wananchi hao, na kuwasihi wananchi kujenga utamaduni wa kuhoji pale ambapo mambo yanapelekwa ndivyo sivyo bila kuogopa wala kumuonea aibu kiongozi yeyote.


Alimalizia kwa kusema kuwa hali bado sio nzuri kwa upande wa wanawake katika uongozi na uwakilishi wa mitaa kwani katika madiwani 14000 nchi nzima wanawake ni 500 tu, ambapo ni sawa na Asilimia 6, huku wanaume wakishika zaidi ya asilimia 90 Katika uongozi.
Muwezeshaji wa Semina inayohusu uwajibikaji katika ngazi serikali za mitaa Geofrey Chambua akitoa ufafanuzi wa jambo fulani kwa washiriki wa semina hiyo.
Mwanaharakati Neema Mwinyi akiwasilisha hali ya uwajibikaji ilivyo katika kata yao ya Mabibo.
Afisa Programu ya Harakati na Ujenzi wa Nguvu za Pamoja Anna Sangai akiongea na washiriki kabla ya kuanza kwa semina.

No comments:

Post a Comment