Thursday, March 16, 2023

HALMASHAURI SIMAMIENI MAKUSANYO NA MATUMIZI YA MAPATO YA NDANI-MHE LONDO


OR-TAMISEMI 

Mwenyekiti wa Kamati ya  Kudumu ya Bunge Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI)  Mhe.Denis Londo  amezitaka Halmashauri zote nchini kuimarisha  usimamizi katika ukusanyaji na matumizi  ya fedha zitokanazo na  mapato ya ndani ili fedha hizo zitumike kutekeleza miradi ya maendeleo na sio kusubiri  fedha kutoka Serikali Kuu.

" Utakuta Halmashauri mapato yake ya ndani  ni Bil. 2 au 3  na katika hali yoyote ile  haiwezi kufikiria kujenga vituo vya afya au shule jukumu hili limebeba Serikali Kuu" Amesema Mhe. Londo

Mhe. Londo ametoa agizo hilo 16 Machi 2023  wakati akihitimisha ziara ya Kamati ya kudumu ya Bunge Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI)  Mkoa wa Simiyu.

Amebainisha  kuwa kuna baadhi ya Halmashauri hazioni  kwamba zina jukumu la kutekeleza miradi ya maendeleo katika Halmashauri zao  hali inayopelekea  kutosimamia ukusanyaji wa mapato ya ndani kwa umakini. 

Aidha amewataka watoa huduma katika vituo vya kutolea huduma za AfyaMsingi nchini kuhakikisha wanatoa huduma bora zinazoendana na uwekezaji ambao unafanywa na Serikali wenye lengo la kuimarisha utoaji wa huduma bora za afya nchini.

Kwa upande wake Naibu Waziri  wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa Mhe. Deogratius Ndejembi ( MB)  amemuelekeza Mkurugenzi wa Idara ya Huduma za Afya, Lishe na Ustawi wa Jamii, Ofisi ya Rais TAMISEMI  kuhakikisha ifikapo tarehe 20 Machi 2023 wataalamu wa kutoa mafunzo ya vifaa tiba wawe wamefika katika Hospitali ya Halmashauri ya Wilaya Bariadi  ili kutoa mafunzo kwa watoa huduma wa hospitali hiyo.

Aidha  amemtaka Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Bariadi kutenga fedha kwaajili ya kujenga njia za watembea kwa miguu ( walkways) katika Hospitali ya Halmashauri Bariadi pamoja na kuhakikisha  anafanya mawasiliano na  Bohari Kuu ya Dawa ( MSD) kuhakikisha generata linafika katika Hospitali ya Halmashauri ya Bariadi na kuanza kufanya kazi.

No comments:

Post a Comment