Tuesday, May 28, 2019

OFISI YA WAKILI MKUU WA SERIKALI YAJIPANGA KUTOA HUDUMA ZENYE UBORA

Na Dennis Buyekwa
Katika kuboresha Sekta ya Sheria na Taifa kwa ujumla, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli, aliona umuhimu wa  kuirudisha tena Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali iliyohamishiwa Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali hapo mnano mwaka 1965.
Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali imeanzishwa kwa Mamlaka aliyo nayo Mhe, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, chini ya Ibara ya 36 (1) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Kwa kuzingatia ibara hiyo, Mhe, Rais alitoa amri ya kuboresha muundo wa Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa  tangazo la Serikali Na. 48 la mwaka 2018 kwa lengo la kuboresha huduma za kisheria katika Sekta ya Umma.
Kufuatia maboresho hayo ya muundo wa Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, mnamo tarehe 13 Februari, 2018, Mhe, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania aliona upo umuhimu wa kuirudisha Ofisi hiyo tena na alisaini Amri ya kuanzishwa kwake, kwa tangazo la Serikali Na. 50 la mwaka 2018.
Aidha Mhe, Rais mnamo tarehe 15 April, 2018 alimteua Dkt. Clement Julius Mashamba kuwa Wakili Mkuu wa Serikali na Dkt. Ally Saleh Possi kuwa Naibu Wakili Mkuu wa Serikali.
Akizungumzia malengo mahususi ya kuirejesha tena Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali, Dkt. Mashamba, alisema urejeshwaji wa Ofisi hii umelenga zaidi katika kuimarisha namna bora ya kuimarisha na kusimamia mashauri mbalimbali yanayoihusu Serikali yaliyo funguliwa na wadau  wa ndani na wale wa nje ya nchi.
‘Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali inao wajibu mkubwa wa kuimarisha na kusimamia kikamilifu kesi zote za madai Mahakamani, katika Mabaraza ya Usuluhishi pamoja na  kesi zote zinazohusu haki za binadamu na zile za kikatiba’.
Malengo mengine ya kuanzishwa kwa Ofisi hii ni pamoja na kuratibu shughuli zote zinazohusu kesi za madai na mwenendo wa usuluhishi kwa niaba ya Serikali Kuu, Mamlaka ya Serikali za Mitaa, Idara mbalimbali zinazojitegemea, na Mashirika ya Serikali, pamoja na kesi zote zinazohusu masuala ya haki za binadamu pamoja na  zile za kikatiba.
Aidha pamoja na malengo hayo mahususi, Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali inaowajibu wa kutekeleza majukumu mbalimbali, ikiwa ni pamoja na kuchukua na kuendesha kesi zote za madai na usuluhishi kwa niaba ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, pamoja na kuwaelekeza Maafisa sheria na Mawakili wa Serikali namna bora ya kusimamia uendeshaji wa kesi hizo.
Dkt. Mashamba aliongeza kuwa Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali inao wajibu wa kuratibu mashauri yote ya madai, haki za binadamu, kesi za kikatiba na usuluhishi katika Mahakama na Mabaraza ya Usuluhishi yanayoihusu Serikali kuu, Idara mbalimbali na Mashirika ya Umma.
Aidha majukumu mengine ya uanzishwaji wa Ofisi hii ni pamoja na kuandaa na  kufungua mashauri mbalimbali kwenye Mahakama za chini, Mahakama Kuu, Mahakama ya Rufaa, na Mabaraza ya Usuluhishi kwa niaba ya Serikali ikiwa ni pamoja na kutoa miongozo kwa wanasheria, mawakili wa Serikali, maafisa na watumishi wengine walioajiriwa katika Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali.
Katika kutekeleza majukumu yake ipasavyo Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali, imedhamiria kuweka utaratibu mzuri kwa kushirikiana na Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali utakao wezesha Wizara, Idara na Taasisi za Umma, kutunza na kutoa taarifa  au kumbukumbu ya kesi za Madai na Usuluhishi zinazosimamiwa katika Wizara, Idara na Taasisi husika ya Umma.
Wakili Mkuu wa Serikali pia alisema tangu kuanzishwa kwa Ofisi hiyo, tayari mashauri 2169 yamesikilizwa katika Mahakama mbalimbali nchini ambapo mashauri 402 ni yale yaliyosajiliwa, 42 ni yaliyosikilizwa katika mabaraza ya ndani na nje ya nchi.
Kwa mujibu wa Wakili Mkuu wa Serikali, mashauri 24 yalihusu masuala ya Katiba na haki za binadamu na mashauri 12 yalihusu maswala mbalimbali ya uchaguzi wakati mashauri 58 yalikuwa ni marejeo na mapitio  ya kesi mbalimbali (Reviews).
Katika kipindi hicho pia Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali ilifanya mazungumzo na Taasisi mbalimbali zenye migogoro na  taasisi nyingine za Setikali kwa pamoja waliweza kutatua migogoro hiyo kwa kila pande kuridhika na suluhu iliyopatikana.
Naye Naibu Wakili Mkuu wa Serikali Dkt. Ally Possi, akizungumza katika mahojiano yaliyofanyika Ofisi kwake Jijini Dar es Salaam, alimshukuru Mhe. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa uamuzi wake wa kuirejesha ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali tangu ilipounganishwa na ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali mwaka 1965.
Dkt. Possi alisema, kuanzishwa kwa Ofisi hii kumeisaidia Serikali kuokoa kiasi kikubwa cha fedha ambazo awali zilitumika kuwalipa Mawakili kwa kuwa Serikali ililazimika kutumia Mawakili wengi binafsi hasa katika kesi za kimataifa kitendo kilichoisababishia hasara kutokana na kuwalipa mawakili hao fedha nyingi tofauti na sasa ambapo Serikali kupitia Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali imekuwa ikiwatumia Mawakili wa serikali hatua iliyosaidia  kuokoa Fedha za Umma.
“Uanzishwaji wa Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali umetimiza azma ya Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika kuhakikisha Serikali yake haitumii fedha nyingi katika uendeshaji wa kesi mbalimbali zilizofunguliwa dhidi ya Serikali ya Tanzania” alisema Dkt. Possi.
Akizungumzia namna ofisi yake ilivyojipanga kushughulikia Mashauri yote kwa wakati, Dkt. Possi alisema kwa sasa wameweka mikakati madhubuti ya ufuatiliaji wa mashauri hayo ikiwa ni pamoja na kushirikiana na Mahakama ili kuweka kipindi maalum cha uendeshaji wa kesi hasa zile zilizokaa muda mrefu kitendo kitakachosaidia kumaliza Mashauri hayo ndani ya muda mfupi.
Katika kuhakikisha wanatoa huduma zenye viwango na ubora Dkt. Possi alisema Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali kwa sasa ina Idara inayosimamia ubora na viwango vya kesi zote zinazoendeshwa na kusimamiwa na Ofisi yake ili kuhakikisha uendeshaji wa Mashauri hayo unakidhi  ubora unaotakiwa.
“Idara hii ina kazi ya kushughulikia na kufuatilia ubora wa Mashauri kitendo kitakachosaidia Mashauri yote yanayoihusu Serikali kusikilizwa muda mfupi ikiwa ni pamoja na kuwasaidia Mawakili kuendesha kesi hizi kwa kuzingatia viwango na ubora unaokubalika” alisema Dkt.Possi.
Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali ilifunguliwa rasmi mkoani Dodoma mnamo Agosti 15, 2018 ambapo hafla hiyo ya ufunguzi ilihudhuriwa na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Majaliwa Kasim Majaliwa pamoja na viongozi waandamizi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

No comments:

Post a Comment