Wednesday, October 24, 2018

SERIKALI YAAINISHA DAWA MUHIMU ZINAZOPATIKANA MSD





SERIKALI kupitia Wizara ya Afya imeainisha dawa aina 135 kama dawa muhimu na za kipaumbele cha wizara  kwa lengo la kuhakikisha kuwa zinapatikana  nyakati zote katika bohari zote za kanda za MSD.

Hayo yameelezwa leo na Waziri wa Afya,Maendeleo ya Janii,Jinsia,Wazee na Watoto Ummy Mwalimu wakati  akitoa taarifa ya utendaji ya Bohari Kuu ya Dawa nchini (MSD)  aliyowasilisha katika kamati ya kudumu ya Bunge huduma na maendeleo ya jamii jijini Dodoma.

Waziri Ummy alisema tathimini ya upatikanaji wa dawa hizo  ni wa hadi mwezi Julai 2018  ambapo ni sawa na asilimia 93 hivyo Wizara yake imeitaka MSD kuongeza idadi ya dawa muhimu 177  na kufikia  dawa za kipaumbele 312 ambapo upatikanaji wa dawa hizo ni asilimia 73 kufikia robo mwaka ya kwanza ya mwaka wa fedha 2018/2019.

“Hali ya upatikanaji dawa muhimu  umeimarika kuanzia mwaka 2016/2017  na kufikia asilimia 93 nchi nzima  katika mwaka 2017/2018  na hivyo kuweza kufanikiwa  katika maeneo mengi na kufikisha  dawa moja kwa moja katika vituo  vya kutolea huduma za afya nchi nzima”.Alisema Waziri Ummy Mwalimu.

Aidha, Waziri Ummy alisema MSD imeweza kusambaza dawa moja kwa moja hadi vituo vya kutolea huduma za afya vinavyofikia 5,432 nchi nzima kwa kutumia magari  215 na hivyo kusambaza dawa zenye thamani za shilingi bilionini 600 kwa mwaka kupitia mfumo wa ugavi ulio enea nchi nzima.

Hata hivyo Waziri Ummy amesema kuwa hivi sasa MSD inapeleka dawa mara 6 kwa mwaka na pale kwenye mahitaji ya dharura tofauti na zamani ambapo ilikua inapeleka dawa mara nne kwa mwaka.

Mbali na hayo Waziri Ummy alisema Bohari ya dawa imeendelea kuimarika kifedha katika kipindi cha miaka mitano iliyopita hususan katika mwaka wa fedha 2017/2018 ambapo Serikali iliongeza bajeti ya dawa, vifaa na vifaa tiba  na kuweza kutoa kiasi cha shilingi bilioni 80.1  na kwa mwaka wa bajeti 2018/2019 kwa robo hii ya mwaka imepokea shilingi bilioni 20.

Kwa upande wake Naibu Waziri wa Afya,Maendeleo ya Jamii, Jinsia,Wazee na Watoto Dkt. Faustine Ndugulile amewataka wafamasia wote wa Hospitali na vituo vya afya kupeleka orodha ya dawa  zilizopo kwenye stoo  kwa madaktari  kila mwanzo wa wiki.

“Wafamasia wote wa Hospitali na zahanati za Serikali wanatakiwa kuwapelekea madaktari orodha ya dawa zilizopo kwenye stoo ili kama dawa ya ugonjwa Fulani haipo Daktari awe na uwezo wa kuandika dawa mbadala kwa mgonjwa” amesema Dkt. Ndugulile.

Naye Mkurugenzi Mkuu wa Bohari ya dawa nchini Bw. Laurean Bwanakunu amesema kuwa katika kuhakikisha upatikanaji wa dawa unadumu nchini wapo katika hatua za mwisho za kukamilisha ubia kati ya Serikali na Sekta binafsi kujenga kiwanda cha dawa nchini.

“Tunatarajia mpaka kufikia Machi 2019 kukamilisha ubia kati ya Serikali na Sekta binafsi kujenga kiwanda cha dawa nchini ambapo utafanyika kwa haraka ili kukamilikia mpaka kufikia mwishoni mwa mwaka 2019” alisema Bw. Bwanakunu.

MWISHO

No comments:

Post a Comment