SERIKALI kupitia Wizara ya Afya imeainisha
dawa aina 135 kama dawa muhimu na za kipaumbele cha wizara kwa lengo la kuhakikisha kuwa
zinapatikana nyakati zote katika bohari
zote za kanda za MSD.
Hayo yameelezwa leo na Waziri wa Afya,Maendeleo
ya Janii,Jinsia,Wazee na Watoto Ummy Mwalimu wakati akitoa taarifa ya utendaji ya Bohari Kuu ya Dawa
nchini (MSD) aliyowasilisha katika
kamati ya kudumu ya Bunge huduma na maendeleo ya jamii jijini Dodoma.
Waziri Ummy alisema tathimini ya upatikanaji
wa dawa hizo ni wa hadi mwezi Julai
2018 ambapo ni sawa na asilimia 93 hivyo
Wizara yake imeitaka MSD kuongeza idadi ya dawa muhimu 177 na kufikia
dawa za kipaumbele 312 ambapo upatikanaji wa dawa hizo ni asilimia 73
kufikia robo mwaka ya kwanza ya mwaka wa fedha 2018/2019.
“Hali ya upatikanaji dawa muhimu umeimarika kuanzia mwaka 2016/2017 na kufikia asilimia 93 nchi nzima katika mwaka 2017/2018 na hivyo kuweza kufanikiwa katika maeneo mengi na kufikisha dawa moja kwa moja katika vituo vya kutolea huduma za afya nchi
nzima”.Alisema Waziri Ummy Mwalimu.
Aidha, Waziri Ummy alisema MSD imeweza
kusambaza dawa moja kwa moja hadi vituo vya kutolea huduma za afya vinavyofikia
5,432 nchi nzima kwa kutumia magari 215
na hivyo kusambaza dawa zenye thamani za shilingi bilionini 600 kwa mwaka
kupitia mfumo wa ugavi ulio enea nchi nzima.
Hata hivyo Waziri Ummy amesema kuwa hivi sasa
MSD inapeleka dawa mara 6 kwa mwaka na pale kwenye mahitaji ya dharura tofauti
na zamani ambapo ilikua inapeleka dawa mara nne kwa mwaka.
Mbali na hayo Waziri Ummy alisema Bohari ya
dawa imeendelea kuimarika kifedha katika kipindi cha miaka mitano iliyopita
hususan katika mwaka wa fedha 2017/2018 ambapo Serikali iliongeza bajeti ya
dawa, vifaa na vifaa tiba na kuweza
kutoa kiasi cha shilingi bilioni 80.1 na
kwa mwaka wa bajeti 2018/2019 kwa robo hii ya mwaka imepokea shilingi bilioni
20.
Kwa upande wake Naibu Waziri wa Afya,Maendeleo
ya Jamii, Jinsia,Wazee na Watoto Dkt. Faustine Ndugulile amewataka wafamasia
wote wa Hospitali na vituo vya afya kupeleka orodha ya dawa zilizopo kwenye stoo kwa madaktari
kila mwanzo wa wiki.
“Wafamasia wote wa Hospitali na zahanati za
Serikali wanatakiwa kuwapelekea madaktari orodha ya dawa zilizopo kwenye stoo
ili kama dawa ya ugonjwa Fulani haipo Daktari awe na uwezo wa kuandika dawa
mbadala kwa mgonjwa” amesema Dkt. Ndugulile.
Naye Mkurugenzi Mkuu wa Bohari ya dawa nchini
Bw. Laurean Bwanakunu amesema kuwa katika kuhakikisha upatikanaji wa dawa
unadumu nchini wapo katika hatua za mwisho za kukamilisha ubia kati ya Serikali
na Sekta binafsi kujenga kiwanda cha dawa nchini.
“Tunatarajia mpaka kufikia Machi 2019
kukamilisha ubia kati ya Serikali na Sekta binafsi kujenga kiwanda cha dawa
nchini ambapo utafanyika kwa haraka ili kukamilikia mpaka kufikia mwishoni mwa
mwaka 2019” alisema Bw. Bwanakunu.
MWISHO
No comments:
Post a Comment