Tuesday, October 31, 2017

JAFO ATEMBELEA KUONA ATHARI KATIKA MIUNDOMBINU MWENDOKASI


Waziri wa nchi, Ofisi ya Rais,Tawala za Mikoa na Serikali za mitaa(TAMISEMI)mhe. Selemani Jafo amewaagiza viongozi wa kampuni ya UDART kufanya kila wawezalo ili ifikapo alhamisi ya wiki ijayo ili kurudisha huduma ya mabasi ya mwendokasi kama ilivyokuwa awali.

Jafo ametoa kauli hiyo leo alipotembelea maeneo tofauti ya huduma ya mabasi ya mwendokasi jijini Dar es salaam na kujionea uharibifu mkubwa wa baadhi ya magari ya mwendokasi uliosababishwa na mafuriko yaliyotokea wiki hii jijini humo.

Katika ziara hiyo, Jafo ameanzia katika kituo cha mabasi cha Kivukoni, na kukagua eneo la Jangwani na kuishia kumalizia ziara yake hiyo katika kituo cha Gerezani. 

Akiwa katika kituo cha Jangwani amebaini uharibifu mkubwa wa zaidi ya mabasi 35 ambayo yameingia maji na kuharibika kwa baadhi ya vipuri ambavyo tayari vimeshaagizwa kutoka Dubai na vinatarajiwa kuingia nchini kuanzia jumanne.

Amesema endapo vifaa hivyo vikifika nchini vitachukua kutwa moja kuvifunga kwa mabasi yote yaliyopata madhara.

Kufuatia hali hiyo, Jafo ameagiza magari hayo ya mwendo kasi kuhamishiwa kwa muda eneo la wazi la Gerezani linalomilikiwa na DART ili kuepusha uharibifu mkubwa wa mabasi hayo endapo mvua zitaendelea kunyesha kwani kwa hali ya sasa eneo la Jangwani sio rafiki kwa kipindi hiki cha mvua.
Jafo amewaagiza DART kuwasiliana na jeshi la polisi jijini humo kuweka utaratibu mzuri katika mataa ili mabasi ambayo hayajapata madhara yaweze kutembea kwa mpangilio mzuri ili kusaidia wasafiri wasikwame vituoni kwa muda mrefu wakati huu ambao magari mengine yanafanyiwa matengenezo ya haraka.

Aidha amemuagiza mtendaji mkuu anaye simamia mradi wa Dar es salaam Metropolitan Development Project  ( DMDP ) kuwasiliana na DAWASA ili wafanye kikao cha haraka waangalie jambo la haraka la kufanya ili kusafisha eneo la chini la mto Msimbazi ili kuondoa tope lililo ziba mifereji ya kupitisha maji kitendo kinacho sababisha maji kusambaa eneo lote la Msimbazi mvua zinaponyesha.

Kadhalika, alisema serikali ipo katika mpango kabambe wa kuliboresha bonde la Msimbazi kupitia mradi wa DMDP unaofadhiliwa na benki ya dunia ambao  wataalam watakuja na namna bora ya kulijenga bonde la Msimbazi ili liweze kupitisha maji yote na kuyapeleka baharini.

No comments:

Post a Comment