SEKRETARIETI ya Ajira katika utumishi wa Umma imesema serikali bado
imesitisha ajira mpya wakati huu ikiendelea kufanya uhakiki wa watumishi
wake pamoja na kupitia upya miundo yake.
Imesema kazi hiyo haijakamilika na kutaka wanaopenda kuajiriwa katika
utumishi wa umma kusubiri mpaka pale watakapotangaza kukamilika kwa
shughuli ya uhakiki.Kauli hiyo imetolewa na katibu wa sekretarieti hiyo, Xavier Daudi jana
wakati akikanusha taarifa ya tangazo la nafasi za kazi zaidi ya 1,000
serikalini lililosambaa mitandaoni.
“Kama mnavyofahamu serikali ilitoa taarifa ya kusitisha kwa muda ajira
mpya serikalini kwa ajili ya kufanya uhakiki wa watumishi wake pamoja na
kupitia upya miundo yake, hivyo mpaka sasa mambo hayo yanaendelea na
hayajakamilika kwa maana usitishwaji wa ajira bado unaendelea,” alisema.
Katibu huyo aliwataka wadau wote kuvuta subira kipindi hiki wakati
uhakiki wa watumishi hewa unapoendelea kufanyika na utakapokamilika na
taarifa rasmi ya nafasi wazi za kazi serikalini itatolewa na mamlaka
husika hivyo wasikubali kupotoshwa na watu wachache .
Alisema kikundi cha watu kwa makusudi wameamua kusambaza taarifa za
uongo katika mitandao ya kijamii kuanzia Septemba 29 kuwa Sekretarieti
ya ajira imetangaza nafasi hizo za kazi zaidi ya 1000, zikiwemo za
Katibu Mkuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii na Mtendaji Mkuu wakala wa
Misitu Tanzania (TFS ) .
Daudi alisema mtu aliyeanzisha uzushi huo aliingia kwenye tovuti ya
Sekretarieti ya ajira na kuchukua matangazo ya Julai 9, mwaka jana, kwa
lugha ya Kiingereza na Kiswahili ambayo yalikuwa na jumla ya nafasi 599
na lingine lilikuwa na nafasi za kazi 513.
Aliwataka wananchi kupuuza taarifa kama hizo za uzushi zinapotokea kwani
matangazo ambayo hutolewa na Sekretarieti hiyo ni lazima yaonekane
kwenye tovuti yake ya www. ajira.go.tz au portal ya ajira ambayo ni
portal. ajira.go.tz .
No comments:
Post a Comment